IQNA

Polisi Nigeria waua Waislamu waliokuwa wakimuomboleza Imam Hussein AS

12:27 - August 24, 2020
Habari ID: 3473097
TEHRAN (IQNA) - Maafisa wa polisi nchini Nigeria wamewashambulia Waislamu waliokuwa wamekusanyika kwa ajili ya maombolezo ya Muharram ya Imam Hussein AS, katika jimbo la Kaduna.

Vyanzo vya habari vimethibitisha kuwa, watu watatu wameuawa shahidi katika hujuma hiyo ya Jumamosi ya askari wa Nigeria dhidi ya waombolezaji wa mjukuu wa Mtume Muhammad SAW,  Imam Hussein AS, Imam wa Tatu wa Waislamu wa madhehebu ya Shia.

Mbali na kuua na kujeruhi kwa mabomu ya gesi ya kutoa machozi, wanajeshi hao wakishirikiana na maafisa wa polisi aidha wamechoma moto gari la wanachama wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria inayoongozwa na Sheikh Ibrahim Zakzaky waliokuwa katika maombolezo hayo jimboni Kaduna.

Mara kwa mara, maafisa usalama wa Nigeria wamekuwa wakiwashambulia kwa silaha za moto Waislamu wakiwa katika shughuli na vikao mbalimbali vya kidini.

Septemba mwaka jana, vikosi vya usalama vya nchi hiyo viliwafyatulia risasi Waislamu walioshiriki katika kumbukumbu ya Ashura na kuwaua shahidi kwa akali waombolezaji 12 na kuwajeruhi makumi ya wengine; huo ni muendelezo wa siasa za chuki na uadui za serikali ya Nigeria dhidi ya Waislamu wa nchi hiyo.

Aidha mwaka 2015, askari wa Nigeria waliwashambulia Waislamu waliokuwa katika maombolezo ya kumbukumbu ya kuuawa shahidi Imam Hussein AS katika mji wa Zaria na kuwaua na kuwajeruhi mamia miongoni mwao. Sheikh Ibrahim Zakzaky, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria pamoja na mkewe walitiwa mbaroni na wanaendelea kuzuiliwa hadi sasa kinyume cha sheria. Wakuu wa Nigeria wamekaidi amri ya mahakama ya kumuachilia huru Sheikh Zakzaky.

3472355

captcha