IQNA

Waandishi habari Sudan walaani kitendo cha kufungwa ofisi ya Al Jazeera

11:01 - January 17, 2022
Habari ID: 3474818
TEHRAN (IQNA)- Waandishi habari nchini Sudan wamelaani vikali kitendo cha wakuu wa utawala wa kijeshi kufunga ofisi za Televisheni ya Kimataifa ya Al Jazeera nchini humo.

Kamati ya Kurejesha Haki za Waandishi Habari wa Sudan imesema kufungwa ofisi ya Al Jazeera ni muendelezo wa ukandamizaji waandishi habari unaotekelezwa na watawala wa kijeshi.

Taarifa zinasema, kibali cha kufanya shughuli za matangazo ya televishen ya al Jazeera Mubasher kimefutwa nchini Sudan kutokana na kile kilichoelezwa na Khartoum kuwa ni kutangaza matangazo yyasiyozingatia utaalamu wa matukio ya Sudan.

Wakili wa Wizara ya Utamaduni na Vyombo vya Habari wa Sudan Nasruddin Ahmad ameamuru kufutwa kibali cha matangazo cha televisheni ya al Jazeera Mubasher huko Khourtoum kwa sababu hiyo iliyotajwa. 

Viongozi wa Sudan wameituhumu ofisi ya televisheni ya al Jazeera mjini Khartoum kuwa inaruhusu kurushwa hewani matangazo ambayo hayajafuata taaluma ya uandishi wa habari kuhusu matukio ya Sudan na kwamba ofisi hiyo inajaribu kuvuruga muundo wa jamii ya Sudan kwa kutangaza habari zinazokiuka kanuni, maadili ya taaluma na lugha ya watu wa Sudan. 

Televisheni ya al Jazeera Mubasher hadi sasa haijatoa jibu lolote kwa hatua hiyo ya Sudan.

Itakumbukwa kuwa, tarehe 30 Mei mwaka 2019 maafisa husika wa Sudan waliifunga ofisi ya televisheni ya al Jazeera lakini miezi miwili baadaye maafisa hao walibadili uamuzi wao huo na kuruhusu tena matangazo hayo. 

Hali si shwari huko Sudan kwani nchi hiyo imeathiriwa na ghasia na mapigano kati ya askari usalama na waandamanaji wanaopinga mapinduzi ya wanajeshi yaliyojiri nchini humo Oktoba 25 mwaka jana. 

Licha ya wanajeshi huko Sudan kuahidi kuwa watakabidhi mamlaka ya uongozi kwa raia lakini wale wanaopinga utawala wa kijeshi nchini humo wanalitaka jeshi kuondoka madarakani na kuundwa serikali halali na ya kidemokrasia nchini humo.  

3477400/

Kishikizo: sudan
captcha