IQNA

Maandamano Afrika Kusini kulaani ubaguzi wa Waislamu nchini India

14:34 - February 26, 2022
Habari ID: 3474979
TEHRAN (IQNA)- Maelfu ya watu kutoka dini zote walikusanyika mjini Johannesburg siku ya Ijumaa kulaani ongezeko la chuki dhidi ya Uislamu na vitisho vya unyanyasaji dhidi ya Waislamu katika baadhi ya maeneo ya India.

Haya yanajiri baada ya kupigwa marufuku kwa hijabu katika vyuo na baadhi ya shule katika jimbo la kusini mwa India la Karnataka mwezi huu jambo ambalo limezua mzozo huku kukiwa na wasiwasi unaoongezeka kwamba mashambulizi dhidi ya nembo na desturi za Waislamu ni sehemu ya ajenda kubwa ya Wahindu ya mrengo wa kulia ya kuwalazimisha walio wachache kufuata itikadi za waliowengi.

Waislamu milioni 200 walio wachache nchini India wanasema kupigwa marufuku kwa hijab kunakiuka uhuru wao wa kidini, unaohakikishwa chini ya katiba ya India.

Mratibu wa maandamano na mwanaharakati wa kijamii Salman Khan amesema vitendo vyovyote vya ubaguzi ni kinyume na maadili ya Uhindu.

"Kuwalazimu wasichana na wanawake nchini India kuvua Hijabu kunaendeleza chuki dhidi ya Uislamu na tunapinga mtu yeyote kubadili desturi zao za kidini," naibu mwenyekiti wa chama cha Congress of Muslim Ummah, ambaye anaongoza katika harakati ya  #handsoffourhijab alisema.

"Hii ni kinyume na mafundisho ya Uhindu na tunatoa wito kwa India iliyoungana, India ya wote ambayo ni kitabu kitakatifu kwa watu wa tamaduni zote kuishi pamoja kwa amani."

Wale waliohudhuria mkutano huo pia waliunga mkono ujumbe huu huku wakiwa wamebeba maandishi ya kuunga mkono Waislamu wanaokabiliwa na ubaguzi na ghasia nchini India.

Khan alisema alikuwa sehemu ya timu iliyoandaa maandamano kwa sababu alihisi kuwa hawezi tena kukaa kimya juu ya suala hilo na kuwataka maafisa wa India kurekebisha hali hiyo.

“Jambo hili limekuwa likitengenezwa kwa muda mrefu nchini India na linaendeshwa na kundi dogo la Wahindu wenye itikadi kali wanaochafua sura ya nchi na sisi tunasema jambo hilo halikubaliki na tunaomba kwa amani hatua zichukuliwe kwani hii ni kinyume cha sheria pamoja na matakwa ya waanzilishi wa India."

Khan aliongeza kuwa idadi kubwa ya Wahindi wanaoishi Afrika Kusini, mojawapo ya idadi kubwa zaidi ya Wahindu  nje ya India, wanaweza kutuma ujumbe wenye nguvu dhidi ya vitendo vyovyote vya unyanyasaji na chuki dhidi ya Uislamu.

"Sisi sote ni kaka na dada na hii ni hali ya hatari sana."

"Tunahitaji kupambana na chuki dhidi ya Uislamu na kuzuia ghasia zaidi ili kila aina ya watu waweze kuishi pamoja kwa amani."

Hali ambayo ilipelekea kuibuka harakati ya kuunga mkono Hijabu ijulikanayo kama  #handsoffourhijab,  ilizidi kuwa mbaya mwanzoni mwa mwezi Februari wakati kundi la wasichana wa Kiislamu waliokuwa wamevalia hijabu walipiga kambi nje ya chuo katika wilaya ya Udupi jimboni Karnataka humo baada ya mamlaka kuwafungia milango.

Hili lilikabiliwa na wimbi kubwa la mshikamano kutoka kote nchini India wakati picha za maandamano hayo zilipoibuka kwenye mitandao ya kijamii kama wanaharakati wakitaka kufutwa kwa marufuku hiyo.

Lakini chuo na serikali hazikutilia maanani maombi hayo na badala yake zilileta athari mbaya, ambapo vyuo vingine kadhaa wilayani humo vilipiga marufuku vazi la hijabu baada ya upinzani kutoka kwa wanafunzi wa Kihindu na wanaharakati waliovalia skafu za rangi ya zafarani,  rangi inayohusishwa na Wahindu wenye misimamo ya kufurutu ada.

3477958

captcha