IQNA

Wanafunzi wa Qur’ani Tukufu Brunei Wakabidhiwa Vyeti

13:18 - May 06, 2026
Habari ID: 3482206
IQNA – Hafla ya utoaji vyeti imefanyika katika Msikiti wa Jamia wa ‘Asr Hassanil Bolkiah nchini Brunei kwa wanafunzi wa madarasa ya Qur’ani Tukufu.

Takriban wanafunzi 70 wa Darasa la Vijana la Juu la Qur’ani la Jame’ ‘Asr Hassanil Bolkiah walitunukiwa vyeti kwa kujitolea kwao kusoma na kuthamini Qur’ani katika hafla iliyofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Matumizi Mbalimbali wa msikiti huo.

Msimamizi wa Msikiti wa Jame’ ‘Asr Hassanil Bolkiah, Haji Haris bin Haji Suboh, ambaye alikuwa mgeni rasmi, ndiye aliyekabidhi vyeti hivyo.

Hafla hiyo, iliyoandaliwa na kamati ya uendeshaji (takhmiri) ya msikiti, ililenga kutambua juhudi na mafanikio ya vijana wanaoshiriki katika madarasa ya juu ya Qur’ani, na pia kuwahamasisha kizazi kipya kuendelea kuzama zaidi katika kuielewa Qur’ani kama mwongozo wa maisha yao ya kila siku.

Madarasa hayo yamepangwa kuwaweka wanafunzi katika misingi ya usomaji sahihi wa Qur’ani, yakiwemo mafunzo ya tarannum (kusoma kwa naghma na lahja za kiqur’ani).

Hafla hii inaonyesha jitihada za msikiti kujijenga si tu kama mahali pa ibada, bali pia kama kituo cha elimu ya Kiislamu na malezi ya tabia njema za vijana wa Kiislamu.

3497336

Kishikizo: brunei qurani tukufu
captcha