IQNA

Iran yalaani mashambulio ya kigaidi Pakistan na Iraq

14:00 - March 28, 2016
Habari ID: 3470218
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani mashambulio ya hivi karibuni za kigaidi katika mji wa Lahore Pakistan na karibu na Baghdad mji mkuu wa Iraq.

Katika taarifa Jumatatu hii, Sadeq Hussein Jaber Ansari Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesisitiza kuwa, mashambulio hayo mawili ya kigaidi, moja katika bustani mjini Lahore na nyingine katika uwanja wa michezo mjini Baghdad ni dalili ya wazi  kuwa magaidi na wenye misimamo ya kufurutu ada hawawajali wala kuwaonea huruma raia  wa kawaida wasio na hatua na kwamba hakuna eneo lolote linalosalimika na uovu wao.

Jaberi Ansari amesema kukaririwa hujuma za kigaidi maeneo mbali mbali duniani ni nukta inayokumbusha kuhusu udharura wa kuchukuliwa hatua za haraka kimataifa ili kukabiliana na tatizo sugu la ugaidi na misimamo mikali.

Ikumbukwe kuwa siku ya Ijumaa magaidi wakufurishaji wa kundi la ISIS au Daesh walishambulia kwa bomu mechi ya soka katika uwanja mmoja mjini Iskanderiyah kusini mwa Baghdad na kupelekea watu wasiopungua 41 kupoteza maisha.

Aidha siku ya Jumapili watu 76 waliuawa na wengine zaidi ya 320 kujeruhiwa kwenye mripuko katika mji wa Lahore, kaskazini mashariki mwa Pakistan. Kundi la kigaidi la Taliban limedai kuhusika na hujuma hiyo iliyopelekea idadi kubwa ya watoto na wanawake kuuawa katika Bustani ya Gulshan Iqbal katika mji huo muhimu nchini Pakistan.

3484711


captcha