IQNA

Baraza la Kiislamu Marekani laanzisha kampeni ya kuwahimiza Waislamu wapige kura

15:05 - January 22, 2020
Habari ID: 3472395
TEHRAN (IQNA) – Baraza la Mahusiano ya Kiislamu Marekani (CAIR) limeanzisha kampeni maalumu ya kuwahimiza Waislamu kushiriki kikamilifu katika uchaguzi wa rais utakaofanyika nchini humo mwaka 2020.

Kampeni hiyo iliyozinduliwa Jumanne 21 Januari inalenga kuimarisha ufahamu wa Waislamu Wamarekani kuhusu uwezo wao wa kisiasa na ushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa 2020 ambao unatazamiwa kufanyika mwezi Novemba.

CAIR inakadiria kuwa kuna Waislamu milioni moja ambao wamejisajili kupiga kura nchini Marekani na idadi kubwa miongoni mwao wako katika majimbo muhimu ambayo huamua hatima ya mshindi wa kiti cha rais.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kitaifa wa CAIR Nihad Awad amesema wanalenga kutumia uwezo mkubwa wa kisiasa wa Waislamu wa Marekani.  Awad ameongeza kuwa: "Uchaguzi Mkuu wa 2020 ni muhimu katika historia ya taia letu na Waislamu Wamarekani. Kuna masuala mengi yanayohusu jamii yetu na uchaguzi huu ni fursa kwa Waislamu kuungana na kufanya kazi pamoja, kujihusisha katika siasa, kujiandikishakupiga kura na kujitokeza kwa wingi kupiga kura kwa njia ambayo haijawahi kushuhudiwa."

Inakadiriwa kuwa, idadi ya Waislamu Marekani mwaka 2017 ilikuwa  ni milioni 3.45 kati ya watu wote milioni 327 nchini humo.

Makadirio yanaonyesha kuwa ifikapo mwaka 2050, idadi ya Waislamu itaongezeka na kufika milioni 8.1 au asilimia 2.1 ya idadi yote ya Wamarekani-na hiyo ni mara mbili ya idadi yao hivi sasa. Uchunguzi umebaini kuwa idadi ya Waislamu Marekani huongezeka kwa takribani laki moja kwa mwaka.

Pamoja na kuwepo ongezeko la chuki dhidi yao, Waislamu wanazidi kuongezeka na hilo linaashiria kuwa kuna watu wengi ambao wanafanya utafiti na kuikumbatia dini tukufu ya Kiislamu maishani huku wakipuuza kauli za kichochezi hasa ambazo zimekuwa zikitolewa na Rais Donald Trump wa nchi hiyo tokea aingie madarakani.

/3873409

captcha