IQNA

WHO yapongeza uamuzi wa Saudia kuhusu Hija

20:31 - June 25, 2020
Habari ID: 3472897
TEHRAN (IQNA) – Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani amepongeza uamuzi wa Saudi Arabia wa kupunguza kabisa idadi ya mahujaji na kuwazuia mahujaji wa kimataifa kuingia nchini humo.

Mkurugenzi wa WHO Tedros Adhanom ametoa taarifa na kusema WHO inaunga mkono uamuzi wa Saudia wa kupunguza idadi ya wanaoshiriki katika Ibada ya Hija, Huku akiutaja mjumuiko wa kila mwaka wa Hija kuwa kati ya mijimuiko mikubwa duniani, Adhanom amesmea uamuzi wa Saudia wa kupunguza kabisa idadi ya mahujaji umeenda kwa mujibu wa maelekezo ya WHO kuhusu kulinda maisha ya mahujaji. Amesema: “Tunadiriki huu haukuwa uamuzi rahisi kwani Waislamu wengi ambao walikuwa wamepanga kutekeleza ibada ya Hija mwaka wamesikitika sana.”

Saudia ilitangaza Jumatatu kuwa ni watu wachache sana watakaoruhusiwa kuhiji mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Hija na Umra ya Saudi Arabia imesema kuwa, Hija ya mwaka huu itashirikisha idadi ndogo ya mahujaji ambao ni raia wa Saudia na raia wa kigeni ambao ni wakazi wa nchi hiyo. Hatua hiyo ya kuwazuia mahujaji kutoka nje ya Saudia imechukuliwa kutokana na kuendelea maambukizi ya ogonjwa wa COVID-19 ambao haujapatiwa chanjo wala dawa.

Mwezi Machi mwaka huu pia Saudi Arabia ilisimamisha ibada ya Umrah kwa Waislamu kutokana na maambukizi ya virusi vya corona. Wakati huo Wizara ya Hija na Umra iliwataka Waislamu kote duniani kusubiri kabla ya kuchukua hatua yoyote ya kujitayarisha kwa ajili ya ibada ya Hija.

3906870

captcha