Ayatullah Sheikh Issa Qassim ameyasema hayo katika hotuba aliyotoa Jumamosi kwa mnasaba wa Usiku wa Ashura na akasisitiza: "Kama tunafuata nyayo za Imam Hussein AS lazima tusimame dhidi ya mapatano na Wazayuni."
Marjaa huyo taqlidi wa Mashia wa Bahrain amesema, huko nchini Bahrain pia kila mwaka vinaendeshwa vita vya kisiasa dhidi ya minbari ya Imam Hussein AS na akongezea kwa kusema: Hii leo pia wafuasi wa Yazid na waungaji mkono wake wamekuwa wakifuata na kuendeleza njia na mwenendo huo.
Katika mikesha kadhaa ya siku za karibuni, vikosi vya usalama vya utawala wa Aal Khalifa nchini Bahrain, kama ambavyo vimekuwa vikifanya kila mwaka vinaposhuhudia mikusanyiko na maandamano ya maombolezo ya Imam Hussein AS, vimewatia nguvuni waongozaji wa maombolezo hayo katika Husainiyya kadhaa na kufunga vipaza sauti vya misikiti na Husainiyya hizo.
Imam Hussein AS, ambaye aliuawa shahidi tarehe 10 Mfunguo Nne Muharram mwaka 61 Hijria katika ardhi ya Karbala nchini Iraq, ametoa funzo na somo la kipekee la kupigania heshima na kukomboka kwa walimwengu wote kutokana na kujitoa kwake mhanga kusio na mfano.