IQNA

Wito wa kuasisiwa kituo cha kukabiliana na maafa katika nchi za Kiislamu

16:07 - October 31, 2020
Habari ID: 3473312
TEHRAN (IQNA)- Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Madhehebu za Kiislamu ametilia mkazo udharura wa kuundwa kituo maalumu cha za Kiislamu kwa ajili ya kukabiliana na maafa katika ulimwengu wa Kiislamu.

Hujjatul Islam Hamid Shahriyari amesema hayo katika mkutano wa 34 wa kimataifa wa Wiki ya Umoja wa Kiislamu unaofanyika kwa njia ya Intaneti na kuongeza kuwa, kuna wajibu kwa Waislamu kushirikiana zaidi na zaidi katika kutatua migogoro iliyopo hivi sasa katika ulimwengu wa Kiislamu. Amesema, kuundwa jopo kazi la pamoja la kutatua migogoro hiyo na kuuongoza ulimwengu wa Kiislamu katika njia sahihi, ni jambo la dharura sana hivi sasa.

Kwa upande wake, Sheikh Waqar Ahmad, mjumbe wa Jumuiya ya Kiislamu ya jimbo la Rajasthan nchini India amesema katika mkutano huo uliofanyika jana usiku kwamba kuna wajibu kwa Waislamu kuwasaidia watu wote wanaokumbwa na matatizo duniani kwani kwa mujibu wa mafundisho ya Uislamu, kuwasaidia watu wengine ni ibada.

Amesema, kuwasaidia watu wengine ni sehemu muhimu ya mafundisho ya Uislamu na kusisitiza kuwa, hivi sasa ambapo walimwengu wanateseka kwa ugonjwa wa COVID-19, Waislamu wako mstari wa mbele kuwasaidia watu wengi ili kwa pamoja iwezekane kuiokoa dunia na janga hili. Amesema hayo ndiyo maadili bora yaliyofundishwa na Mtume Muhammad SAW.

Mkutano wa 34 wa kimataifa wa Umoja wa Kiislamu ulianza juzi Alkhamisi tarehe 29 Oktoba 2020 kwa njia ya Intaneti na utaendelea hadi keshokutwa Jumatatu. Zaidi ya wasomi na wanachuoni 160 wakubwa wa ulimwengu wa Kiislamu kutoka nchi 47 duniani wanashiriki katika mkutano huo. Washiriki wanaunganishwa kwa njia ya video kutokea nchini Iran.

Mkutano wa kimataifa wa umoja wa Kiislamu hufanyika kila mwaka kwa munasaba wa Wiki ya Umoja wa Kiislamu. Inafaa kuashiria hapa kuwa Wiki ya Umoja wa Kiislamu ni kipindi cha kati ya tarehe 12 na 17 za Mfunguo Sita Rabiu Awwal kipindi ambacho kinasadifiana na kuadhimisha Maulidi na kumbukumbu ya kuzaliwa Bwana Mtume SAW. Kuhusiana na kuzaliwa Bwana Mtume SAW kuna riwaya mbili mashuhuri. Waislamu wengi wa madhehebu ya Kisuni wanaamini kwamba, Bwana Mtume SAW alizaliwa tarehe 12 Mfunguo Sita Rabiul Awwal mwaka wa tembo uliosadifiana na mwaka 570 Miladia.

Kundi jengine la Waislamu ambalo linaundwa zaidi na Waislamu wa madhehebu ya Shiia Ithanaashari linaamini kwamba, Mtume wa Uislamu alizaliwa tarehe 17 Mfunguo Sita Rabiul Awwal mwaka huo huo. Mitazamo hiyo miwili takribani pengo lake ni kipindi cha wiki moja. Kwa kuzingatia hali hiyo, Imam Ruhullah al-Musawi al-Khomeini (MA) Mwasisi na Mwanzilishi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran akakitaja kipindi hiki cha wiki moja kuwa Wiki ya Umoja, ili Waislamu badala ya kuvutana na kuanza kukuza tofauti za tarehe za kuzaliwa Bwana Mtume SAW wakae pamoja na kujadili umuhimu wa umoja na changamoto mbalimbali zinazowakabili Waislamu na ulimwengu wa Kiislamu kwa ujumla.

 

3932158

 

captcha