Kwa mujibu wa taarifa kijana huyo aliyeuawa shahidi ametambuliwa kama Mohammad Ali Khabisa na alipoteza maisha baada ya kulengwa kichwani na askari katili wa Israel wakati wa maandamano ya amani ya kila wiki ya kupinga ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika mji wa Beita kusini mwa Nablus, siku ya Ijumaa.
Wizara ya Afya ya Palestina imesema Mpalestina huyo aliyekuwa na umri wa miaka 28 amepoteza maisha kwa kupigwa risasi na jitihada za kuokoa maisha yake zilifeli hata baada ya kukimbizwa kituo cha afya.
Hilali Nyekundu ya Palestina huko Nablus imetangaza kuwa, waandamanaji wengine sita walijeruhiwa katika tukio hilo baada ya askari wa utawala dhalimu wa Israel kuwapiga risasi za plasitiki huku wengine 18 wakipata matatizo ya kupumua baada ya kurushiwa gesi ya kutoa machozi.
Kwa mujibu wa takwimu, kuna walowezi wa Kizayuni wapatao 650,000 wanaoishi katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Quds (Jerusalem) Mashariki.
Kwa mujibu wa azimio nambari 2334 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, shughuli zote za Israel za ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni ni kinyume cha sheria. Hata hivyo utawala wa Kizayuni unakaidi marufuku hiyo, kila leo unavunja nyumba za Wapalestina, kuwapora ardhi na mashamba yao na kujenga vitongoji haramu vya walowezi wa Kizayuni bila ya kuchukuliwa hatua yoyote na Umoja wa Mataifa.