Kwa mujibu wa Dar al-Maaref, Waziri wa Wakfu wa Misri, Sheikh Osama al-Azhari, amethibitisha kuwa mashindano hayo yatafanyika katika mwezi wa Kiislamu wa Jumada al-Thani 1447, unaolingana na katikati ya mwezi Desemba mwaka huu.
Pia, alitangaza kwamba ametoa idhini rasmi ya kuipa jina la Shahat Anwar mashindano ya mwaka huu kwa heshima ya mchango wake mkubwa katika huduma ya Qur’ani.
Shahat Anwar, aliyefariki mwaka 2008, alijulikana sana kwa usomaji wake wa Qur’ani uliokuwa na hisia kali na mguso wa kiroho. Sauti yake iliwasisimua Waislamu kote duniani, na mtindo wake wa kusoma Qur’ani bado unatumiwa kama marejeo na wanafunzi pamoja na wasomaji wa Qur’ani.
Mashindano ya mwaka huu yatakuwa na makundi mbalimbali yanayolenga kuhifadhi na kusoma Qur’ani, yakiwemo tafsiri, Tajwidi, na muktadha wa kihistoria wa aya. Pia, kutakuwa na makundi maalum kwa wasiosoma Kiarabu, watu wenye ulemavu, na familia zinazojihusisha na Qur’ani.
Mashindano haya ya kimataifa ya Qur’ani nchini Misri hufanyika kila mwaka, yakikusanya wasomaji na wahifadhi bora wa Qur’ani kutoka mataifa mbalimbali. Zaidi ya washiriki 100 na majaji kutoka zaidi ya nchi 60 walihudhuria mashindano ya mwaka jana.
3493028