IQNA

Kiongozi Muadhamu apongeza ikhlasi na jitihada za shahidi Fakhrizadeh

16:10 - January 26, 2021
Habari ID: 3473591
TEHRAN (IQNA) - Familia ya mwanasayansi bingwa na mwenye kipawa cha juu katika masuala ya nyuklia na ulinzi wa Iran shahidi Mohsen Fakhrizadeh jana ilimtembelea Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei.

Katika mkutano huo, Ayatullah Khamenei alimuenzi shahidi Fakhrizadeh kwa kipawa kikubwa alichokuwa nacho katika masuala ya kisayansi na kiufundi na jinsi mwanasayansi huyo mwenye hadhi ya juu alivyokuwa na hima na bidii kubwa mno katika medani ya elimu na matendo; na akasema: daraja ya juu ya hadhi ambayo Mwenyezi Mungu amempa kwa kumruzuku kufa shahidi ndio malipo ya ikhlasi na uchapajikazi wake ulio nadra kushuhudiwa; na daraja hiyo haiwezi kulinganishwa na hadhi na cheo chochote kile cha kidunia.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamua amesema, kuwa na adhama jina la shahidi Fakhrizadeh mbele ya wananchi, na vijana wengi kusikitika kwa kutopata kumjua wakati wa uhai wake ni katika athari nyingine za ikhlasi aliyokuwa nayo.

Aidha, Ayatullah Khamenei ameihutubu familia ya shahidi Fakhrizadeh: "wake wa mashahidi wana fungu katika malipo ya thawabu zao; na tunamuomba Mwenyezi Mungu aziteremshie nyoyo zenu subira na utulivu; na kwa taufiki yake, muweze kuendelea kuwa na mwenendo unaoendana na hadhi ya yeye shahidi."

Katika mkutano huo, mke na watoto wa shahidi Mohsen Fakhrizadeh walimshukuru Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kwa ujumbe wake wa upendo na huruma na wa utaalamishaji aliotoa baada ya kuuawa kigaidi shahidi Fakhrizadeh na wakasisitizia haja ya kubainishwa harakati ya kifikra ya mashahidi wa jihadi ya elimu na kufanywa kuwa mfano wa kuigwa.

Dakta Mohsen Fakhrizadeh, aliyekuwa Mkuu wa Shirika la Utafiti na Uvumbuzi la Wizara ya Ulinzi ya Iran na mmoja wa wanasayansi bingwa wa sekta ya nyuklia nchini aliuawa shahidi Novemba 27, 2020 katika shambulio la kigaidi viungani mwa mji mkuu, Tehran.

3473809

captcha