IQNA

Yemen yasema itaendeleza hujuma ndani ya Saudia hadi Wasaudi wasitishe uvamizi

18:04 - March 01, 2021
Habari ID: 3473692
TEHRAN (IQNA) - Mjumbe wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Answarullah ya Yemen amesisitiza kuwa, harakati hiyo itaendelea kuishambulia miji na maeneo ya Saudi Arabia maadamu uko wa Aal Saud unaendelea kuishambulia miji ya Yemen.

Televisheni ya al Mayadeen imemnukuu Muhammad al Bukheiti akisema hayo jana na kuongeza kuwa, operesheni za makombora dhidi ya Saudia zitaendelea hadi pale dola hilo vamizi litakapoacha mashambulizi na kuizingira Yemen kila upande. Amesema, hiyo itakuwa hatua ya kwanza na ni baada ya hapo ndipo San'a itakuwa tayari kufanya mazungumzo ya kuutafutia ufumbuzi wa kisiasa mgogoro huo ulioanzishwa na Saudi Arabia.

Mjumbe huyo wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Answarullah ya Yemen pia amesema, kuzingirwa kila upande nchi hiyo ni hatari zaidi kuliko hata mashambulizi ya kijeshi. Hata hivyo amesema, inashangaza kuiona serikali mpya ya Marekani inaitaka San'a isiendelee kujihami wakati Yemen bado imezingirwa kila upande huku Saudi Arabia ikiendeleza mashambulio yake kila uchao dhidi ya wananchi wasio na hatia wa Yemen.

Aidha amesema, Answarullah inashambulia maeneo ya kijeshi ndani ya Saudi Arabia na itaendelea na mashambulizi yake, hivyo wananchi wa nchi hiyo wanapaswa kukaa mbali na maeneo hayo.

Juzi Jumamosi, jeshi la Yemen na vikosi vya kujitolea vya wananchi wa nchi hiyo vilishambulia kwa kombora na ndege kadhaa zisizo na rubani, maeneo muhimu ya Riyadh, mji mkuu wa Saudi Arabia.

Yemen inasema kuwa ni haki yake kujihami kutokana na uvamizi wa Saudi Arabia na magenge yake na maadamu uvamizi huo ungalipo, miji ya Saudia nayo haitobaki salama.

3474117

Kishikizo: yemen saudi arabia
captcha