Mohammad Baqer Qalibaf amesema katika ujumbe alioutoa kabla ya kuanza kikao cha Bunge hii leo kwamba, anawatakia kheri Wakristo wa Iran na duniani kiujumla katika sherehe zao za kukumbuka kuzaliwa Nabii Isa (Yesu) mwana wa Maryam Amani ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake.
Spika wa Bunge la Iran amesema: Natoa mkono wa baraka kwa Wakristo na wapenda haki kote duniani na hasa raia wenzangu wa Iran wa dini ya Kikristo kwa mnasaba wa maadhimisho ya siku ya kuzaliwa Nabii Isa AS.
Kuna Wakristo zaidi ya 120,000 wanaoishi hapa nchini Iran. Akthari yao ni Waarmenia wanaofuata madhehebu ya Kikristo ya Othodoksi.
Wakristo kote duniani hii leo wanaadhimisha sikukuu yao ya Krisimasi wanayoinasibisha na siku ya kuzaliwa Nabii Isa Masih AS, sherehe ambazo hufanyika tarehe 25 Disemba kila mwaka.
Wakatoliki na Waprotestanti huadhimisha Krismasi Disemba 25, huku Waothodoksi wakiadhimisha kumbukumbu ya mazazi hayo ya Isa Masih (AS) Januari 7.
Isa Masih (AS) ni mmoja wa Mitume wakubwa wa Mwenyezi Mungu ambaye ametajwa kwa heshima na taadhima kubwa katika Qur'ani Tukufu, na inamtambulisha kama mmoja wa Manabii wakuu waliopewa Kitabu na sheria na Mwenyezi Mungu.
4109402