IQNA

Al Azhar yakosoa vikwazo dhidi ya Russia na kupuuzwa jinai za utawala wa Israel

17:35 - March 02, 2022
Habari ID: 3474995
TEHRAN (IQNA)- Chuo cha Kiislamu cha Al Azhar nchini Misri kimekosoa vikwazo vya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) dhidi ya Russia wakati shirikisho hilo linapuuza jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel na kusema hiyo ni ishara ya wazi ya undumakuwili.

Al Azhar imetoa taarifa hiyo baada ya FIFA na Shirikisho la Soka Ulaya, UEFA, kutangaza kupiga marufuku timu ya taifa ya soka ya Russia na vilabu vyote vya nchi hiyo kushiriki katika michezo ya kimataifa kutokana na oparesheni za kijeshi za nchi hiyo huko Russia.

Kufuatia uamuzi huo wa FIFA, Al Azhar imehoji hivi: "Je mnaijua Palestina" Ubinadamu haugawanyiki wakati wa vita na migogoro."

Al Azhar imeendelea kusema: "Haipasi kutumia sera za undumakuwili. Tunalaani hatua ya FIFA hasa kwa kuzingatia kuwa shirikisho hilo kwa muda mrefu  limekuwa likipuuza kadhia ya Palestina kwa kudai kuwa siasa hazipaswi kuingizwa katika michezo."

Tarehe 24 mwezi ulioisha wa Februari, Rais Vladimir Putin wa Russia alitoa amri ya kutekeleza oparesheni maalumu ya kijeshi Ukraine na kusisitiza kuwa, Moscow haina nia ya kukalia kwa mabavu ardhi ya nchi yoyote ile.

Operesheni hiyo ilianza siku chache baada ya Russia kutangaza kutambua rasmi uhuru wa majimbo mawili ya Donestk na Luhansk ya mashariki mwa Ukraine.

Russia inasema Ukraine imevunja makubaliano ya Minsk ya mwaka 2014 na 2015 kati ya Kyiv na majimbo yanayopigania uhuru wao na kwamba Ukraine ndiyo iliyoanza kutumia nguvu za kijeshi kushambulia majimbo yaliyojitangazia uhuru.

Hivi sasa Russia inasema Ukraine inapaswa kupokonywa silaha na iwe nchi isiyofungamana na upande wowote.

4039929

captcha