IQNA

Sayyed Nasrallah: Marekani ndiyo chanzo kikuu cha mgogoro wa Ukraine

20:27 - March 01, 2022
Habari ID: 3474990
TEHRAN (IQNA)- Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon Sayyed Hassan Nasrallah ametoa hotuba muhimu katika ufunguzi wa kongamano linalofanyika mjini Beirut kwa mnasaba wa kumbukumbu ya mwaka wa 30 tangu alipouawa shahidi Katibu Mkuu wa Pili wa Hizbullah, Sayyid Abbas al-Musawi na kusema Marekani inabeba dhima ya mgogoro wa sasa wa Ukraine.

Sayyid Abbas al Musawi, ambaye ni mmoja wa waasisi wa Hizbullah ya Lebanon aliuawa shahidi tarehe 16 Februari 1992 pamoja na mkewe Ummu Yasir na mwanawe Hussein katika shambulio la kigaidi la helikopta ya Apachi ya utawala haramu wa Kizayuni wa Israel. Wakati huo Sayyid Abbas alikuwa ndiye Katibu Mkuu wa harakati hiyo ya muqawama.

Katika hotuba ya ufunguzi  wa kongamano hilo lililofanyika kwa anuani ya "Bwana wa Mashahidi Wetu; Fikra na Sira" Sayyid Hassan Nasrallah amesema: "Ni wajibu wetu kutunza kubukumbu za fikra asili, hatua kubwa za kujitoa mhanga na ukweli wenye adhama wa harakati za wapiganaji wa muqawama na kuhakikisha hotuba na mijadala yote inayohusiana na kongamano hili vinahifadhiwa katika sura ya kitabu na nyaraka zinazokubalika."

Katibu Mkuu wa Hizbullah ameashiria pia vita na mapigano yanayoendelea hivi sasa baina ya Russia na Ukraine na akasema: baada ya kuanza shambulio la Russia dhidi ya Ukraine, baadhi wameunga mkono, baadhi wamelaani na wako pia waliotangaza kutopendelea upande wowote. Lililo muhimu hapa ni kufuatilia tukio hilo linalojiri duniani na kupata somo na funzo kutokana na kila saa na siku yake.

Sayyid Hassan Nasrallah ameongeza kuwa, Marekani ndio inayobeba dhima ya matukio yanayojiri hivi sasa nchini Ukraine, kwa sababu inachochea mapigano hayo na wala haijasaidia kupatikana njia za kidiplomasia na kusimamishwa vita, bali zaidi ilishinikiza ili vita hivyo vianze.

Katibu Mkuu wa Hizbullah amegusia na kuunga mkono pia hotuba iliyotolewa leo na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyed Ali Khamenei kuhusu mapigano yanayoendelea kati ya Russia na Ukraine; na akasema: Marekani imefanya kila njia kwa ajili ya kufanikisha yale yanayoshuhudiwa hivi sasa na inaandaa mazingira ya kuifanya hali hiyo iwe tata zaidi. Yanayojiri hii leo ni funzo kwa watu wanaoiamini Marekani.

4039648

captcha