IQNA

Mtaalamu kutoka Iran kujiunga na Jopo la Majaji wa Mashindano ya Kimataifa ya Qur’an Malaysia

15:27 - July 22, 2025
Habari ID: 3480981
IQNA – Kwa mara ya kwanza baada ya karibu miongo miwili, mtaalamu wa Qur’an Tukufu kutoka Iran atahudhuria kama jaji katika mashindano ya kimataifa ya Qur’an nchini Malaysia.

Mtaalamu na mwalimu mashuhuri wa Qur’an Tukufu, Ustadh Gholam Reza Shahmiveh, atahudumu katika jopo la majaji wa toleo la 65 la mashindano haya mashuhuri katika eneo la Asia ya Kusini.

Kwa mujibu wa Kituo cha Masuala ya Qur’ani cha Taasisi ya Wakfu na Masuala ya Hisani ya Iran, mwaliko rasmi kwa mtaalamu huyu anayeheshimika kimataifa ulipokelewa siku chache zilizopita. Hivyo basi, baada ya karibu miaka ishirini, kutakuwepo tena jaji kutoka Iran katika mashindano haya ya kimataifa ya Qur’an, yanayojulikana kama ya zamani kabisa duniani.

Maafisa wa kituo hicho wametaja ushawishi wa ujumbe wa Iran uliozuru Malaysia mwezi Desemba mwaka jana, pamoja na mchango mkubwa wa hayati Ustadh Abdolrasoul Abaei katika matoleo yaliyopita, kuwa sababu kuu za mwaliko huu.

Ustadh Abaei, aliyefariki mwezi Aprili mwaka huu, ndiye alikuwa Muirani wa mwisho na wa pekee kuwahi kushiriki kwenye jopo la majaji la mashindano haya ya Qur’an ya kimataifa nchini Malaysia.

Toleo la 65 la Mashindano ya Kimataifa ya Usomaji na Kuhifadhi Qur’an ya Malaysia (MTHQA) litaanza rasmi tarehe 2 Agosti 2025 katika Kituo cha Biashara cha Dunia Kuala Lumpur (WTCKL), na litadumu hadi tarehe 9 Agosti.

Jumla ya washiriki 72, wakiwemo mahafidh na wasomaji wa Qur’an, kutoka nchi 50 wanatarajiwa kushiriki kwenye mashindano haya ya kihistoria.

Kwa upande wa Iran, Qari Mohsen Qassemi atawakilisha nchi yake katika kipengele cha usomaji (tilawa) katika mashindano haya ya heshima kubwa duniani.

3493933

Habari zinazohusiana
captcha