
Osama Raslan, msemaji wa Wizara ya Awqaf ya Misri, ametangaza kuwa taifa hilo litakuwa mwenyeji wa fainali kuanzia tarehe 6 hadi 10 Desemba.
Ameeleza kuwa mashindano haya ni makubwa zaidi ya aina yake duniani, kama ilivyoripotiwa na gazeti la Al-Dustour.
Katika mahojiano ya simu na kipindi cha “Hadha Sabah” kilichorushwa na Extra News, Raslan alifafanua kuwa upekee wa mashindano ya mwaka huu ni idadi isiyokuwa na mfano ya washiriki 158 waliofika katika hatua ya mwisho, baada ya mchujo wa awali uliowahusisha mamia na hata maelfu ya waombaji kutoka mataifa mbalimbali duniani.
Msemaji huyo alibainisha kuwa matumizi ya teknolojia ya kisasa yamewezesha raundi za awali kufanyika kwa njia ya mbali na kuhakikisha kuwa ni wagombea waliobobea pekee wanaoendelea hadi hatua ya mwisho.
Amesema mashindano haya yanashuhudia ushiriki wa nchi 72, idadi kubwa zaidi katika historia ya tukio hili la Qur’ani.
Raslan amesisitiza kuwa msaada wa serikali ya Misri uko katika kiwango cha juu kabisa, akibainisha kuwa rais wa nchi huwatunuku washindi binafsi kila mwaka katika usiku wa Laylatul-Qadr ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Aidha, ameeleza kuwa jumla ya zawadi za mwaka huu inafikia paundi milioni 13 za Kimasri.
Raslan ameongeza kuwa duru hii ya mashindano inalingana na mafanikio ya mpango wa “Hali ya Tilawa” uliozinduliwa na Wizara ya Awqaf kwa lengo la kugundua vipaji vya Wamisri katika tilawa ya Qur’ani.
Amesisitiza kuwa upekee wa mashindano unatokana na roho ya Kimasri, kwani hayahusishi tu kuhifadhi Qur’ani, bali pia ustadi wa qira’at mbalimbali, ufahamu wa sarufi, sababu za kushuka kwa aya, na tafsiri yake.
Ameeleza kuwa lengo ni kuandaa washiriki watakaokuwa mabalozi wa Qur’ani, wenye uwezo wa kusoma aya kwa usahihi na kuelewa maana zake.
3495604