Katika taswira hiyo, Sayyed Nasrallah anazungumza kuhusu mkutano huo akisema ulifanyika jioni ya Januari 1, 2020. Wawili hao walizungumza kuhusu matukio ya kieneo. "Alikuwa ametulia na mwenye yakini. Alikuwa na mtazamo chanya sana," amesema Nasrallah.
Katika kikao hicho, Shahidi Soleimani pia alishiriki katika Swala ya Jamaa iliyoongozwa na Sayyed Nasrallah.
Ikumbukwe kuwa, Luteni Jenerali Qassem Soleimani, Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) alielekea Iraq Januari 3 mwaka 2020 kufuatia mwaliko rasmi wa wakuu wa Iraq.
Punde baada ya kuwasili Iraq aliuawa shahidi katika hujuma ya ndege za kivita za jeshi vamizi na la kigaidi la Marekani karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad. Aidha katika hujuma hiyo ya kigaidi Abu Mahdi Al Muhandis, Naibu Mkuu wa Harakati ya Kujitolea ya Wananchi wa Iraq, naye pia aliuawa shahidi akiwa ameandamana na Qassem Soleimani. Watu wengine wanane waliokuwa katika msafara huo nao pia waliuawa shahidi.
Shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani alikuwa na nafasi kubwa katika mapambano na maadui pamoja na magaidi na pia katika kuangamiza kundi la kigaidi la Daesh au ISIS. Pia alikuwa nguzo muhimu katika harakati za kupigania ukombozi wa Palestina. Halikadhalika alikuwa na nafasi muhimu katika kusambaratisha njama ya Marekani na Wazayuni ya kuligawa eneo vipande vipande.