IQNA

Mbunge Muislamu Marekani, Ilhan Omar, apinga sera za Trump dhidi ya Iran

20:26 - January 09, 2020
Habari ID: 3472356
TEHRAN (IQNA) - Mbunge Muislamu Marekani apinga sera za Trump dhidi ya Iran na kusema vikwazo na vita vya kiuchumi ni hatua ambazo zinakinzana na sera za kupunguza taharuki.

Mbunge wa chama upinzani cha Democrats katika Baraza la Wawakilishi la Bunge la Kongresi la Marekani Bi Ilhan Omar ambaye ni Mmarekani mwenye asili ya Somalia aliwasilisha muswada katika bunge ili kumzuia rais Trump kutumia nguvu za kijeshi dhidi ya Iran bila idhini ya bunge.

Wajumbe wengi katika Kongresi walilaani vikali hatua ya Rais Donald Trump kutoa amri ya kutekeleza shambulizi ambalo lilimuua Luteni Jenerali Qassem Soleimani, Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu na hivyo kuzidisha tahruki baina ya Iran na Marekani.

"Ukweli usemwe: mauaji ya Qassem Soleimani yalikuwa ni kitendo cha vita ambacho kilichukuliwa bila idhini ya Kongresi, hatua ambayo ni ukikwaji wa Katiba ya Marekani," alisema Omar.

Aidha katika ujumbe wa Twitter siku ya Jumatano, Omar amesema "vita huharibu maisha na kusambaratisha mustakabali wa vizazi. Nilipata funzo hilo nikiwa na umri mdogo wa miaka 8.  Watu duniani na Marekani wanataka tuchukue hatua tafauti mara hii. Hatutaki vita na Iran."  Bi. Omar amesema watoto wengi Iraq na Afghanistan wanafahamu madhara ya vita.

Ihlan ambaye alikuwa mkimbizi baada ya vita kuibuka Somalia alikimbilia nchini Kenya na kuishi na familia yake katika kambi la wakimbizi ya Dadaab akiwa na umri wa miaka 8 kuanzia mwaka1991 hadi 1995 kabla ya kuhamia Marekani.

Luteni Jenerali Qassem Soleimani, Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC, Ijumaa Alfajiri 3 Januari aliwasili nchini Iraq kufuatia mwaliko rasmi wa wakuu wa nchi hiyo. Punde baada ya kuwasili, akiwa ndani ya gari pamoja na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu Kamanda wa kikosi cha kujitolea cha wananchi wa Iraq maarufu kama al Hashd al Shaabi pamoja na watu wengine nane, walishambuliwa kwa anga na wanajeshi vamizi na wa kigaidi wa Marekani karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad na wote walikufa shahidi katika tukio hilo.

Siku ya Jumatano, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC limezipiga kwa makumi ya makombora, kambi mbili za Marekani nchini Iraq ikiwa ni kujibu jinai ya kigaidi iliyiofanywa na askari vamizi wa Marekani ya kumuua shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani.

Mara baada ya Marekani kumuua kigaidi na kidhulma Luteni Jenerali Soleimani, vyombo vya habari vya nchi hiyo na vya Magharibi viliendesha propaganda kubwa ya vita vya kisaikolojia huku rais wa Marekani akitoa vitisho kwamba atapiga vituo 52 muhimu vya Iran, vya kiutamaduni, kisiasa, kijeshi, kiuchumi n.k, kama Iran italipiza kisasi. Lakini baada ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuipiga Marekani kibao kikali cha uso, viongozi wa White House wameshindwa kuficha kutapatapa kwao na baada ya kuchukuka muda mrefu na kuakhirisha mara kadhaa hatimaye Donald Trump jana jioni alijitokeza mbele ya waandishi wa habari na kurudia tuhuma zile zile za kila siku dhidi ya Iran, akatoa ahadi zile zile za kila siku za kuiwekea vikwazo zaidi Iran na hakuzungumzia kabisa vitisho alivyotoa siku chache tu zilizopita.

3870446

captcha