IQNA

Mashindano ya Kimataifa ya Qur'an Misri: Wizara ya Wakfu yatangaza tarehe ya mchujo

18:16 - July 18, 2025
Habari ID: 3480959
IQNA – Wizara ya Wakfu ya Misri imetangaza majina ya washiriki wa KiMisri waliokidhi masharti ya kushiriki katika mtihani maalum wa uteuzi, ili kuwachagua wawakilishi katika toleo la 32 la mashindano ya kimataifa ya Qur'an nchini humo, pamoja na tarehe ya mtihani huo.

Kwa mujibu wa tovuti ya An-Naba, mtihani huu maalum wa mdomo kwa ajili ya kuwapata wawakilishi wa Misri utaanza Jumapili, tarehe 20 Julai 2025, na utaendelea hadi tarehe 27 Julai.

Wale watakaofanya vizuri zaidi katika mtihani huu ndio watakaopewa heshima ya kuiwakilisha Misri katika mashindano hayo matukufu.

Wizara ya Wakfu imezielekeza idara zake zote zinazohusika kuwajulisha washiriki juu ya umuhimu wa kuhudhuria mtihani huu saa nne kamili asubuhi (10:00 AM).

Toleo la 32 la Mashindano ya Kimataifa ya Qur'an la Misri linatarajiwa kufanyika mwezi Disemba 2025, kwa heshima ya kumuenzi na kumkumbuka Al-Marhum Ustadh Shahat Muhammad Anwar – qari maarufu wa Misri na ulimwengu wa Kiislamu.

Misri hufanya mashindano haya kila mwaka, yakiwa ni jukwaa la kimataifa linalowaleta pamoja washiriki kutoka pembe mbalimbali za dunia.

Lengo la mashindano haya ni kukuza utamaduni wa Kiislamu na kuhimiza usomaji na hifadhi ya Qur'an Tukufu. Toleo la mwaka jana lilihudhuriwa na washiriki zaidi ya 100 pamoja na majaji kutoka nchi 60. Mashindano hayo yalikuwa na  kategoria mbalimbali za qiraa na hifdhi.

Kila toleo la mashindano haya limekuwa likifanyika kwa heshima ya kuwakumbuka baadhi ya maqari maarufu wa Misri kama vile Sheikh Mahmoud Khalil Al-Husary, Sheikh Abdul Baset Abdul Samad na wengineo – Allah awaridhie na awape daraja ya juu Jannatul Firdaus.

3493873

Habari zinazohusiana
captcha