Dar al-Ifta, mamlaka rasmi ya fatwa nchini Misri na iliyo chini ya Al Azhar, ilitoa tamko kupitia ukurasa wake rasmi wa Facebook, ikijibu swali kuhusu uhalali wa kugawa zakat kwa familia za mashahidi wa Gaza, kwa mujibu wa Arabi 21.
Tamko hilo lilieleza kuwa zakat kiasili ilifaradhishwa “kwa ajili ya kujenga utu wa binadamu na kutimiza mahitaji yao ya msingi.” Likaongeza: “Iwapo suala linahusu kuokoa maisha na kuwalinda watu dhidi ya njaa, kiu na maradhi, kama ilivyo kwa watu wa Gaza ,basi ni halali, kwa mujibu wa sheria ya Kiislamu, kuelekeza na kuhamisha mali ya zakat kwao. Hakuna pingamizi katika hili.”
Dar al-Ifta ilisisitiza kuwa michango hiyo lazima itolewe “kupitia njia rasmi, halali na zilizoidhinishwa” ili kuhakikisha kuwa mali hiyo inawafikia wale wanaostahiki kwa haki.
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Palestina huko Gaza, tangu tarehe 7 Oktoba 2023, takriban watu 67,869 wameuawa na wengine 170,105 wamejeruhiwa katika mashambulizi ya Israel. Idadi kubwa ya waathirika ni wanawake na watoto. Wizara hiyo pia ilibainisha kuwa zaidi ya watu 9,500 bado hawajulikani walipo, huku hali ya njaa ikishaua maisha ya Wapalestina 463, wakiwemo watoto 157.
Fatwa hiyo imetolewa wakati ambapo kuna usitishaji tete wa mapigano huko Gaza, baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kutangaza makubaliano ya kusitisha mashambulizi siku ya Alhamisi. Harakati ya Kiislamu ya Kupigania Ukombozi wa Palestina inayokulikana kwa kifupi kama Hamas na Israel wamebadilishana wafungwa kama sehemu ya hatua ya awali ya makubaliano hayo.
Mazungumzo hayo yalifanyika katika mji wa Sharm el-Sheikh nchini Misri, yakisimamiwa na Marekani, huku yakiratibiwa na nchi za Uturuki, Misri na Qatar.
Licha ya miito ya mara kwa mara ya kimataifa na maamuzi ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki kuhimiza usitishaji wa mapigano, mashambulizi ya Israel, kwa himaya Marekani, yaliendelea, yakisababisha ukimbizi mkubwa, njaa na uharibifu wa hali ya juu
3495012