
Msikiti Mkuu wa Algiers, kwa ushirikiano na Wizara ya Mambo ya Nje kupitia Idara ya Jamii ya Algeria Nje ya Nchi, siku ya Ijumaa uliandaa programu maalum kwa ajili ya vijana 52 Waalgeria wanaoishi ughaibuni, gazeti la Al-Shorouk linaripoti.
Katika ratiba hiyo, wageni walitembelea sehemu mbalimbali za Msikiti Mkuu wa Algiers na taasisi zake za kielimu na kitamaduni. Pia kulifanyika kikao cha kielimu kwa lugha ya Kiarabu, Kiingereza na Kifaransa, kilichoshirikisha maprofesa na maimamu wa msikiti, kujadili misingi ya mamlaka ya kidini ya Algeria na sifa zake za wastani.
Sehemu ya kuvutia zaidi ilikuwa usomaji wa pamoja wa Surah Al-Kahf na wanafunzi kabla ya Sala ya Ijumaa katika uwanja wa msikiti.
Ratiba ilihitimishwa kwa mkutano na Sheikh Muhammad Al-Ma’moon Al-Qasimi Al-Husani, Imam wa Msikiti Mkuu wa Algiers.
Msikiti huu, ulioko mashariki mwa mji mkuu Algiers, ni wa tatu kwa ukubwa katika ulimwengu wa Kiislamu baada ya Msikiti Mtukufu wa Makka na Msikiti wa Mtume (SAW) mjini Madina. Minara yake, inayotazamika kutoka kila kona ya jiji, ndiyo minara mirefu zaidi duniani kwa urefu wa mita 267.
Minara hiyo ina ghorofa 43 na lifti. Jengo lote, lenye usanifu wa Kiislamu wa Algeria na ukumbi wa sala, lina ukubwa wa hekta mbili na lina uwezo wa kuwahudumia waumini 120,000 pamoja na maegesho ya magari 2,000.
4325279