
Kundi hilo limerekodi ongezeko hilo la mara 11 la matukio yanayowalenga Waislamu katika miezi mitatu ya kwanza ya mwaka huu pekee.
Ripoti hiyo ya sera ya Mpac, yenye kichwa “The Pitfalls of Operation Epic Fury: How the Undeclared War Against Iran Hurts Americans’ Interests Abroad and at Home” (Mitego ya Operesheni Hasira ya Hamasa: Jinsi Vita Dhidi ya Iran Vinavyodhuru Maslahi ya Wamarekani Nje na Ndani ya Nchi), inaeleza kuwa angalau mashambulizi tisa yalitokea mwezi Machi pekee, yakihusisha uharibifu wa mali, vitisho vya mabomu misikitini, na hata unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake Waislamu.
Khuram Zaman, Mkurugenzi mwanzilishi wa Kituo cha Usalama, Teknolojia na Sera katika Mpac, aliliambia tovuti ya Middle East Eye (MEE): “Jambo moja tunaloweza kubainisha ni kwamba vita dhidi ya Iran vilianza mwishoni mwa Februari, na ndilo tunaloamini kuwa msingi wa mgawanyiko kati ya hali tuliyoiona mwaka 2025 na hali tunayoishuhudia sasa.”
Aliongeza: “Imekuwa jambo la kawaida sana kuzungumzia Waislamu kwa dharau. Mazungumzo ya kuchoma misikiti au kutumia vilipuzi (IED) misikitini si vitu ambavyo ungevitazamia kuona kwenye mitandao ya kijamii. Ghafla, tangu kuanza kwa vita dhidi ya Iran, imekuwa kama jambo linalokubalika kwa watu kutumia aina hiyo ya lugha.”
Mwezi uliopita, Kituo cha Utafiti wa Chuki Iliyopangwa (CSOH) kiliripoti kuwa kilifuatilia machapisho yaliyokuwa yakivunjia utu, kubagua, na kuchochea ghasia dhidi ya Waislamu kuanzia Januari 1 hadi Machi 5, na kubaini “ongezeko kubwa” la machapisho hayo kwenye jukwaa la X (zamani Twitter) ya Elon Musk, saa chache baada ya vita dhidi ya Iran kuanza.
Yaliyomo katika machapisho hayo yanahusu mambo mengi, kuanzia maoni ya kibinafsi yaliyojaa chuki hadi wito kwa wabunge kutunga sera kali za ubaguzi, ikiwa ni pamoja na “Sheria ya Kuwatenga Waislamu” (Muslim Exclusion Act) na kuwafukuza Waislamu wote nchini.
Ripoti ya Mpac inaonyesha kuwa lugha hiyo ya chuki pia inatoka kwa wabunge wa chama cha Republican, jambo linalofanya hali hiyo ionekane kama ya kawaida. Mwakilishi wa Florida, Randy Fine, amekuwa mstari wa mbele kwa wito wake wa kumfukuza meya Mwislamu wa Jiji la New York, Zohran Mamdani, huku akidai: “Ikiwa watatulazimisha kuchagua, chaguo kati ya mbwa na Waislamu si gumu.”
Mbunge mwingine, Andy Ogles wa Tennessee, ameweka wazi imani yake kuwa “Waislamu hawastahili kuwa katika jamii ya Marekani.” Wabunge wote wawili ni wanachama wa kundi jipya la “Sharia-Free America,” ambalo sasa lina zaidi ya wanachama 60 kutoka chama tawala cha kihafidhina cha Republican.
Zaman aliliambia MEE: “[Kundi hili] sasa ni kubwa kuliko kundi la wabunge wa asili ya Kihispani, ni kubwa kuliko ‘Freedom Caucus’, na nadhani lina ukubwa sawa na kundi la wabunge wenye asili ya Afrika (Congressional Black Caucus). Wanachama wa kundi hili wametoa wito wa kuwavua uraia na kuwafukuza Waislamu kutoka Marekani, hatua ambayo ni sawa na usafishaji wa kikabila (ethnic cleansing).”
‘Kudhoofisha asasi za kiraia’
Ripoti ya Mpac inaonyesha kuwa hisia za chuki dhidi ya Waislamu si jambo geni tangu baada ya mashambulizi ya 9/11, lakini hofu kuu ni jinsi zinavyozidi kukubalika katika jamii.
“Kihistoria, vipindi vya ushiriki mkubwa wa kijeshi wa Marekani Mashariki ya Kati vimekuwa vikifuatana na ongezeko la chuki dhidi ya Waislamu, ikichochewa na mabadiliko ya jinsi vyombo vya habari na wanasiasa wanavyowasilisha masuala hayo ili kupata uungwaji mkono wa umma kwa ajili ya mizozo,” ilisema ripoti hiyo.
Hata hivyo, Mpac inaonya: “Dhana kwamba kupunguza haki za Waislamu wa Marekani kunaongeza usalama wa taifa haina mashiko; kinyume chake, inahatarisha kuondoa imani, ushirikiano, na mshikamano wa kijamii ambao ndio msingi wa usalama wa kweli.”
Mpac inasisitiza wito wake wa kusitishwa kabisa kwa vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran, ikionya kuwa vita hivyo vitahuisha na kupanua mbinu za kikati za kiusalama za ndani zinazokumbusha kipindi cha baada ya 9/11, ikiwemo ufuatiliaji mkali wa jamii za Waislamu na kupanuliwa kwa mamlaka ya uchunguzi ya Idara ya Kitaifa ya Upelelezi, FBI.
“Hatua kama hizi kijadi zimekuwa zikifuatiwa na mmomonyoko wa uhuru wa kiraia… na kudhoofisha asasi za kiraia,” ripoti hiyo ilihitimisha.
Mpac imetoa wito kwa utawala wa Trump na taasisi za umma kuchukua hatua za “kukemea haraka lugha na matendo yote ya chuki, kuwawajibisha wahalifu wa ghasia, na kushirikiana kikamilifu na jamii zilizoathirika ili kuelewa na kujibu mahitaji yao.” Hata hivyo, Zaman alionya kuwa hadi makampuni ya mitandao ya kijamii yatakapoanza “kuchukua mambo haya kwa uzito” na kudhibiti akaunti zinazochochea taarifa za uongo na vitisho vya ghasia, Waislamu wa Marekani hawatakuwa salama.
3497123