Sayyid Abbas Araghchi ameishukuru Iraq, serikali yake, wananchi wake, viongozi wa kidini (Marja’iya), na vyombo vya usalama kwa mapokezi ya dhati waliyoyatoa kwa mwili mtakatifu wa Ayatullah Khamenei, na kwa heshima kuu iliyoambatana na ibada za mazishi ya Kiongozi huyo Shahidi wa Ummah.
Araghchi amesema kuwa mahusiano kati ya Iran na Iraq si jambo la kawaida la mipaka ya kijirani au adabu za kidiplomasia pekee, bali yamejengeka juu ya historia ndefu ya pamoja, maadili yanayofanana, na hatima moja iliyounganishwa.
“Iraq ni ardhi ya ukarimu na uthabiti, na tunawashukuru kwa kusimama nasi katika kipindi hiki cha majonzi,” alisema.
Waombolezaji wa Iraq walianza kuwasili Najaf kabla ya mapambazuko ya jua siku ya Jumatano, na kufikia adhuhuri, mamilioni walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya msafara huo wa mazishi, wakijaza mitaa ya jiji hilo katika maonesho ya huzuni na mshikamano. Matukio hayo yamebaki kuwa moja ya vituo muhimu zaidi katika safari ya mazishi hayo nchini Iraq.
Makabila ya Iraq yaliupokea mwili wa Kiongozi Shahidi Sayyid Ali Khamenei kwa nara za kijadi, baada ya kuwasili sambamba na miili ya mashahidi wengine katika “Barabara ya Hussein” (inayojulikana pia kama barabara ya Najaf-Karbala), njia kuu ya watembea kwa miguu inayounganisha miji mitakatifu ya Najaf na Karbala nchini Iraq.
“Kile walichokionyesha kaka na dada zetu wapendwa wa Iraq kupitia mapokezi yao ya hamasa, ukarimu wao mkubwa, na ushiriki wao wa ajabu wa mamilioni ya watu katika msafara wa mazishi ya Kiongozi Shahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu, kilikuwa ni dhihirisho lisilo na mfano wa heshima, ukarimu, na udugu wa Kiislamu,” Araghchi aliongeza.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesisitiza kuwa: “Maonesho haya ya ajabu ya mshikamano yameakisi uhusiano wa kina wa kidini, kihistoria, na kiutamaduni kati ya mataifa haya mawili ya Kiislamu ya Iran na Iraq, uhusiano ambao umesalia thabiti kupitia mapenzi ya Imam Hussein (AS), na kwa mara nyingine umedhihirisha ukweli usioyumba kwamba ‘Hubb al-Husayn Yajma’una’ (‘Mapenzi kwa Imam Hussein yanatuunganisha’) mbele ya macho ya dunia nzima.”
“Hakuna shaka kwamba yale yaliyojiri katika miji mitakatifu ya Najaf na Karbala yamekuwa sura nyingine ya dhahabu katika historia ya mahusiano ya kindugu na kirafiki kati ya Iran na Iraq, mahusiano ambayo yamejikita katika maadili ya Kiislamu, imani ya pamoja, na vifungo visivyoweza kuvunjika kati ya mataifa haya mawili,” alihitimisha mwanadiplomasia huyo mkuu wa Iran.
3498171