Rais Pezeshkian ameyasema hayo katika ujumbe wake wa leo Alhamisi kwa taifa la Iran, wakati wa maandalizi ya hafla za kumwaga na kumzika Imam Khamenei, ambaye aliuawa shahidi mnamo Februari 28, siku ya kwanza ya vita vya kichokozi Marekani na Israel dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu.
Rais ameonyesha imani yake kuu juu ya nafasi ya wananchi katika kipindi hiki cha mabadiliko, akibainisha kuwa katika hafla hii adhimu ya mazishi, taifa la Iran litathibitisha tena utiifu wake kwa njia na malengo makuu ya Kiongozi huyo aliyeawa shahidi.
Rais amesisitiza kuwa ushiriki wa wananchi katika tukio hili la kihistoria utathibitisha, bila shaka yoyote, uaminifu wao kwa njia iliyowekwa na marehemu Kiongozi.
Ameongeza kuwa kifo cha kishahidi cha Ayatullah Khamenei kimeacha simanzi nzito si tu miongoni mwa Wairani, bali pia katika ulimwengu wa Kiislamu na mataifa yote yanayopigania uhuru. Hata hivyo, amesisitiza kuwa pigo hilo limefunua ukweli usiopingika kwamba misingi imara ya mfumo wa Kiislamu imejengeka juu ya “nguzo madhubuti za imani, malengo matukufu, na utashi wa taifa kubwa.”
Rais Pezeshkian ameusifu upeo wa mawazo na utendaji wa Shahidi Imam Khamenei katika kulinda uhuru wa Iran, huku akikuza demokrasia ya kidini na utamaduni wa muqawama (mapambano) katika baadhi ya vipindi vyenye changamoto kubwa zaidi katika historia ya kisasa ya taifa la Iran.
Amesema kuwa jina, mawazo, na mafanikio ya Shahidi Ayatullah Khamenei bila shaka yatasalia milele katika kumbukumbu ya kihistoria ya taifa la Iran na dhamiri ya watu wote wanaopigania haki duniani kote.
Rais ametoa wito kwa Wairani wote, bila kujali kabila, dini, au mwelekeo wa kisiasa, kujitokeza kwa wingi katika shughuli za mazishi ili kuonesha taswira ya umoja wa kitaifa na uaminifu kwa malengo matukufu ya mfumo wa Kiislamu.
4361700