Siku ya Jumamosi, Jumuiya ya Waislamu wa Assunnah huko Ottawa iliandaa soko la kila mwaka la Idul Adha na tamasha.
Sikukuu ya Kiislamu ya Idul Adha ambayo huandamana na msimu wa ibada ya Hija hujumuisha sala ya Idi ya jamaa, mikusanyiko mikubwa ya kijamii na kutoa kwa wale wanaohitaji.
Tukio la Jumamosi katika Msikiti wa Rehema lilikuwa na wachuuzi na maduka ya vyakula, pamoja na eneo la watoto kucheza nje. Ilikuwa sherehe ya kwanza ya Idul Adha hadharani katika msikiti huo tangu janga la Corona lilipoanza.
Amer Al-Nabelseya na Dina Mohamed, ambao wanafanya biashara ya upishi kutoka nyumbani, waliweza kuuza kwa wingi keki aina ya knafeh, ambayo ni kitafunia cha jadi cha mataifa kadhaa ya Mashariki ya Kati.
Al-Nabelseya alisema kiungo chao cha siri katika keki hizo tamu ni upendo.
"Mnapofanya chakula kwa nia njema na moyo safi na kwa mapenzi, kitaakisi katika ladha yake," alisema.
Uislamu ni dini inayoenea kwa kasi zaidi Canada ambapo Waislamu wameongezeka kwa asilimia 82 katika kipindi cha muoongo moja uliopita. Hivi sasa Waislamu ni asilimia 3.2 ya watu wote milioni 35 nchini Canada.
Disemba mwaka 2017, Waziri Mkuu Justin Trudeau katika ujumbe wake kwa Kongamano la Kuhuisha Uislamu alisema Waislamu nchini Canada wamekuwa na mchango mkubwa na ni rasilimali muhimu kwa nchi.
"Canada ina bahati kuwa na jamii ya Waislamu wenye harakati," alisema Trudeau katika ujumbe wake maalumu kwa njia ya video.
"Kwa muda wa miaka mingi, Waislamu nchini Canada wameweza kupata ustawi na kutoa mchango mkubwa kwa jamii huku wakiwa wanadumisha ufungamano muhimu na nchi zao za asili na jambo hilo limewawezesha kuwa na turathi nzuri ya utamaduni."
Pamoja na kuwa Waislamu ni jamii muhimu nchini Canada lakini wamekuwa wakikabiliwa na changamoto za wenye chuki dhidi ya Uislamu ambao hutekeleza mashambulizi ambayo yamepelekea Waislamu kadhaa kuuawa na misikiti kuharibiwa.