Ahmed Al-Qadidi, Balozi wa nchi hiyo ya Afrika Kaskazini nchini Qatar, alitoa maoni hayo katika makala iliyochapishwa kwenye tovuti ya Arabi21. Zifuatazo ni nukuu za makala yake:
Harakati ya wanafunzi wa vyuo vikuu vya Marekani na Ulaya kuunga mkono Wapalestina wa Gaza imekuja wakati shakhsia wasomi wa Kiyahudi pia wamelaani vita vya utawala wa Kizayuni dhidi ya Ukanda wa Gaza na ukatili ambao umekuwa ukifanya.
Ni wazi kwamba vita dhidi ya Gaza, vilivyoanza tarehe 7 Oktoba, vimebadilisha mpangilio usio wa haki wa siasa za kimataifa. Huu ni mpangilio ambao ulikuwa umejikita kwenye uwongo na upotoshaji wa ukweli na watu wamezoea kukubalika.
Katika kipindi cha wiki chache zilizopita, wanafunzi wa vyuo vikuu vya Marekani na maprofesa wamepandisha bendera ya Palestina katika vyuo vikuu, wakafanya vikao na kutoa wito wa kukomeshwa mauaji ya kimbari ya utawala ghasibu wa Israel huko Gaza na kusitishwa uungaji mkono wa nchi yao kwa vita vya kikatili dhidi ya Wapalestina.
Mikutano na vikao vimeenea hadi vyuo vikuu kote Marekani na nchi nyingine za Magharibi, ikiwa ni pamoja na Ufaransa.
Kumekuwa na dalili za mabadiliko makubwa katika jinsi wanafunzi wa vyuo vikuu pamoja na wasomi wanavyoona matukio ya kimataifa. Siku chache zilizopita, mwanazuoni na mwanafalsafa wa Ufaransa aliyekuwa akiiunga mkono Israel alisema kwa mara ya kwanza kuwa utawala wa Kizayuni unaelekea kudidimia na kuangamizwa.
Harakati za sasa za wanafunzi wa vyuo vikuu katika nchi za Magharibi ni ukumbusho wa uasi wa wanafunzi dhidi ya rais wa Ufaransa Charles de Gaulle mwaka 1968, ambao ulileta mabadiliko makubwa katika jamii ya Ufaransa na Ulaya kwa kauli mbiu kama "urafiki badala ya vita".
Leo, wanafunzi wameinuka nchini Ufaransa dhidi ya mauaji ya Wapalestina.
Mtu anapaswa kukumbuka kuwa Ufaransa ndiyo nchi pekee ambayo ina sheria ya ajabu ambayo kuhoji takwimu zilizotajwa kuhusu mauaji ya Holocaust kunaweza kukuweka jela.
Huku maandamano ya wanafunzi wa vyuo vikuu vya Marekani yakiendelea kufanyika kwa lengo la kupinga jinai za utawala wa Kizayuni huko Gaza na vilevile kwa ajili ya kuwaunga mkono Wapalestina, polisi wa nchi hiyo wameongeza hatua zao za ukandamizaji dhidi ya wanafunzi hao.
Maandamano makubwa na yasiyo na mfano wake yanaendelea kufanyika katika vyuo vikuu vya Marekani kwa lengo la kuwaunga mkono Wapalestina na kupinga vitendo vya jinai vya utawala wa Israel, na hivyo kuashiria mabadiliko ya kimsingi na muhimu katika mtazamo wa kizazi cha vijana wa Marekani kuhusu suala zima la Palestina.
/3488250