IQNA

Umoja wa Kidini

Mchungaji nchini Misri agawa peremende kwenye Milad-un-Nabi

20:04 - September 15, 2024
Habari ID: 3479438
IQNA - Mchungaji Mkristo nchini Misri amesambaza peremende au pipi za bure miongoni mwa watu katika hafla ya Milad-un-Nabi ya kuadhimisha kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (SAW).

Yuanis Adib, mchungaji Mkristo wa Kanisa la Kopti, amesema analenga kukuza mshikamano na urafiki kati ya Wakristo na Waislamu wa nchi hiyo ya Kiislamu.

Alitoa peremende miongoni mwa watu, hasa wafanyakazi wa ujenzi na wafagia barabara katika mji wa Hurghada katika Jimbo la Bahari ya Sham nchini Misri.

Amesema siku ya kuzaliwa Mtume Muhammad (SAW) ni tukio la baraka na fursa kwa Wakristo wa Misri kushiriki katika sherehe za ndugu zao Waislamu.

"Kama vile Waislamu hushiriki katika sherehe za Wakristo wa Kopti, sisi, Wakristo huhudhuria sherehe za Kiislamu ili kufikisha ujumbe wa urafiki na udugu," alisema.

Watu wa Misri, Wakristo na Waislamu, wana nia ya kuimarisha urafiki na uhusiano wa kindugu katika hafla za kidini, Adib aliongeza.

Wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani mapema mwaka huu, pasta huyo huyo alisifiwa kwa kusaidia kusambaza milo ya Iftar kwa wahitaji.

Misri ni nchi ya Afrika Kaskazini yenye wakazi wapatao milioni 104. Asilimia 90 ya watu wa nchi hiyo ni Waislamu.

Wakopti wa Misri ndio jumuiya kubwa zaidi ya Kikristo katika ulimwengu wa Kiarabu. Makadirio ya idadi yao nchini Misri hutofautiana, lakini kwa ujumla ni kati ya milioni 4.7 na 7.1.

3489902

Habari zinazohusiana
captcha