IQNA

Wafungwa Wapalestina wasusia chakula kulalamikia udhalimu wa Israel

22:15 - July 16, 2021
Habari ID: 3474105
TEHRAN (IQNA)- Wafungwa watano Waplaestina wameanza mgomo wa kususia chakula katika magereza ya kuogofya ya utawala wa Kizayuni wa Israel kama kwa lengo la kulalamikia kushikiliwa gerezani bila ya kubainika makosa yao.

Taarifa zinasema wafungwa wanne miongoni mwao wanashikiliwa katika gereza la Rimon kaskazini mwa ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu (Israel) na mwingine anashikiliwa katika gereza lililo katika jangwa la Negev.

Wafungwa hao wanalalamika kuwa wanashikiliwa gerezani bila kubainika sababu za kufungwa au kufahamishwa tarehe ya kuachiliwa huru.

Idara ya Masuala ya Wafungwa Wapalestina inasema vifungo hivyo ni ukiukaji wa wazi wa haki za binadamu kwani ni haki ya wafungwa kufahamu sababu yakushikiliwa na muda watakaoshikiliwa. Karibu wafungwa 540 Wapalestina katika jela za Israel wanashikiliwa bila kujua tuhuma  zinazowakabili na pia hawajafahamishwa watashikiliwa kwa muda gani.

Kwa ujumla  hivi sasa kuna wafungwa 4,650 Wapalestina wanaoshikiliwa katika magereza ya kuogofya ya Israel.

Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) imekuwa ikiwateka nyara Waisraeli ili kuushinikiza utawala haramu wa Israel uwaachilie huru wafungwa Wapalestina.

Mwaka 2011, utawala  wa Kizayuni wa Israel ulilazimika kuwaachilia huru wafungwa 1,000 Wapalestina, akiwemo kiongozi wa sasa wa Hamas Yahya Sinwar, mkabala wa kuachiliwa huru Gilad  Shalit, mwanajeshi wa Israel ambaye alikuwa ameshikiliwa mateka Ghaza kwa zaidi ya miaka mitano.

3475255

captcha