IQNA

Msikiti wa Los Angeles ulioteketea kwa moto kujengwa upya

23:25 - January 17, 2025
Habari ID: 3480067
IQNA – Kufuatia moto mbaya huko Los Angeles, California nchini Marekani ambao umeuteketeza Msikiti wa At-Taqwa, jamii ya Waislamu imekusanya zaidi ya dola 745,000 kwa ajili ya kujenga upya msikiti huo.

Baada ya moto wa Eaton wa Januari 7, 2025, kampeni rasmi ya kujenga upya msikiti huo tayari imekusanya zaidi ya dola 745,000, na lengo la uchangishaji limeongezwa hivi karibuni ili kuruhusu michango zaidi, kulingana na kampeni ya Launchgood. "Kampeni hii ni kampeni rasmi iliyoidhinishwa na kudhaminiwa na bodi ya Masjid Al-Taqwa," waandaaji walisisitiza, wakihimiza umma kuendelea na msaada wao wa ukarimu.

Kwa zaidi ya miaka 20, Masjid Al-Taqwa umekuwa zaidi ya sehemu ya ibada kwa jamii za Altadena, Pasadena, na maeneo jirani. "Masjid Al-Taqwa umekuwa zaidi ya sehemu ya sala—ni nyumbani kwa wengi wetu," alisema Backer Abu-Jaradeh, mkandarasi mkuu na mhandisi wa umeme anayeongoza juhudi za ujenzi upya.

Msikiti umehudumu kama kitovu cha imani, mikusanyiko ya jamii, na huduma muhimu, na kueteketea kwake kumeumiza hisia za wengi sana.

Juhudi za Ujenzi Mpya

Mradi wa ujenzi unafanywa na Bayt Construction, ambayo imejitolea kufanya kazi kwa gharama, kuhakikisha kila dola iliyotolewa inatumika kwenye kazi na vifaa. "Hakutakuwa na faida ya mkandarasi au malipo—ni gharama tu za kujenga upya," Abu-Jaradeh aliwahakikishia wafadhili.

Ili kusisitiza uwazi zaidi, michango yote inapelekwa kwenye akaunti rasmi ya msikiti. Kwa wale wanaotafuta uhakikisho zaidi, waandaaji wamependekeza mawasiliano na wanachama wa bodi ya Masjid Al-Taqwa au Imam, Junaid.

Wimbi la Msaada

Majibu kutoka kwa jamii yamekuwa ya aina yake. Lengo la awali la uchangishaji limezidi kutokana na idadi kubwa ya misaada inayooendelea kutolewa, na waandaaji wamelazimika kuruhusu watu zaidi kuchangia. "Huu ni wakati wetu wa kurudisha," inasema taarifa ya kampeni hiyo. "Msikiti wa Masjid Al-Taqwa umekuwa hapo kwa ajili yetu—sasa ni zamu yetu kuungana na kuhakikisha unasimama tena imara."

Eneo la California linapoendelea kupambana na moto wa kuharibu, hadithi kama hizi zinaonyesha uvumilivu wa imani na jamii. Ujenzi upya wa Masjid Al-Taqwa unasimama kama ushahidi wa roho ya kudumu ya waumini wake na ukarimu wa wale wanaojali kuhifadhi nafasi za ibada na umoja.

3491481

captcha