Akizungumza pembezoni mwa shughuli ya kuaga mwili wa Kiongozi huyo Shahidi, Ziyad al-Nakhalah alisema: “Ayatullah Khamenei alikuwa kiongozi wa kipekee aliyewapenda watu wa Palestina; na kwa upande wao, Wapalestina na wapiganaji wa Muqawama walilipa mapenzi hayo na uaminifu huo.”
Amesisitiza kuwa kuuawa kwake shahidi ni hasara kubwa kwa Ummah wa Kiislamu, lakini wakati huo huo ni ishara ya heshima na fahari kuu katika njia ya jihadi.
Nakhaleh ameeleza kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imekuwa daima msaidizi mkuu wa watu wa Palestina na vikosi vya Muqawama, akiongeza kuwa msimamo huu ni muendelezo wa njia ya Imam Khomeini (RA) na Kiongozi Shahidi, ambao utaendelea chini ya uongozi wa Jamhuri ya Kiislamu hadi malengo ya Ummah na kadhia yake kuu yatakapotimizwa.
“Msimamo wa kuunga mkono Muqawama utaendelea, na Jamhuri ya Kiislamu itabaki kuwa msaidizi mkuu wa watu wa Palestina,” alisisitiza.
Akibainisha kuwa urithi wa Kiongozi Shahidi utadumu kupitia muendelezo wa msimamo wa Muqawama, alisema kuwa Muqawama wa Palestina utaendelea katika njia yake maadamu utawala ghasibu (wa Israel) upo katika ardhi ya Palestina, na kwamba vikosi hivyo havitarudi nyuma katika chaguo lao hadi ushindi utakapopatikana.
3498098