IQNA

Meya wa Kwanza Mwislamu kuchukua usukani wa New York wiki hii

13:17 - December 29, 2025
Habari ID: 3481734
IQNA – Zohran Mamdani ataapishwa kuwa meya wa 110 wa Jiji la New York wiki hii, ambapo ataweka historia kwa kuwa Mwislamu wa kwanza kuliongoza jiji kubwa zaidi nchini Marekani.

Mamdani, mwenye umri wa miaka 34, aliendesha kampeni kwa misingi ya sera za Kisoshalisti za Kidemokrasia, akiahidi kushughulikia gharama kubwa za maisha jijini. Ahadi kuu ni kusimamisha ongezeko la kodi ya nyumba kwa zaidi ya milioni moja ya vyumba. Pia ameahidi kujenga nyumba za bei nafuu 200,000 na kutoa huduma ya malezi ya watoto kwa wote, ingawa maelezo kamili bado hayajafafanuliwa.

Sherehe ya kuapishwa itafanyika usiku wa kuamkia Mwaka Mpya, ambapo Mwanasheria Mkuu Letitia James ataongoza kiapo. Seneta Bernie Sanders wa Vermont atasimamia hafla ya mchana nje ya Jumba la Jiji.

Licha ya tofauti za kisiasa, mkutano wake wa Novemba na Rais wa Marekani Donald Trump ulikuwa wa heshima ambapo Trump alilegeza msimamo na kukubali kuwa Mamdani ni meya wa New York.

Maafisa wa uhamiaji wa shirikisho wamekuwa wakiongeza shughuli zao jijini, jambo linaloweza kuwa kitovu cha mvutano. Wasifu wa kisiasa wa Mamdani ni mfupi, ukiwa na muhula mmoja tu kama mwakilishi wa Bunge la Jimbo. Ili kufidia, amejizungushia wasaidizi wazoefu kutoka tawala zilizopita na kufungua mazungumzo na viongozi wa biashara waliokuwa wakitabiri uhamaji wa matajiri.

Kama mtetezi wa haki za Wapalestina, meya huyu Mwislamu mwenye asili ya India na ambaye alizaliwa Uganda, anakabili jukumu la kuwahakikishia Wayahudi uongozi shirikishi. Hivi karibuni, mfanyakazi mmoja alijiuzulu baada ya kufichuliwa ujumbe wa chuki dhidi ya Wayahudi aliowahi kuandika miaka iliyopita.

“Kwa kawaida meya wa New York huwa ni alama ya kitamaduni,” alisema Profesa Lincoln Mitchell wa Chuo Kikuu cha Columbia.

Wakazi wa New York pia wameona uungaji mkono wa dhati wa Mamdani kwa mkewe, msanii wa Kisyria Rama Duwaji. Akaunti yake ya Instagram imepata zaidi ya wafuasi milioni moja tangu Novemba.

3495886

Habari zinazohusiana
Kishikizo: new york meya mwislamu
captcha