
Ofisi ya kisiasa ya Hizbullah imeeleza wasiwasi wake kuhusu sera za kuchupa mipaka za Washington dhidi ya nchi za eneo hili, ikimkosoa mtawala wa Marekani, Donald Trump kwa kutishia kuangamiza mataifa ya eneo na kubadilisha serikali zao, televisheni ya Al Manar imeripoti.
"Uchokozi wa Marekani dhidi ya mataifa na watu katika eneo letu umefikia kiwango cha kiburi, na hata kutishia maisha ya Kiongozi Mkuu wa Kidini wa mamilioni ya Waislamu, Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei," imesema.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa, "Hili linatishia kuwasha moto katika eneo lote, na kuongeza tisho dhidi ya wananchi wa Iran ambao wamesimama kidete dhidi ya majaribio ya Marekani na Wazayuni ya kudhoofisha usalama na utulivu wao."
Kambi hiyo ya wabunge ya Harakati ya Hizbullah ya Lebanon imesisitiza kuwa, inasimama upande wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, watu wake, na uongozi wake.
Aidha imempongeza Ayatullah Khamenei kwa "uongozi wake wa busara na ushujaa," ikisema, Kiongozi Muadhamu anayapa matumaini mataifa yaliyokandamizwa, katika juhudi zao za kukabiliana na dhulma duniani kote.
Habari inayohusiana:
Kadhalika Ofisi ya Kisiasa wa Harakati ya Muqawama ya Hizbullah katika Bunge la Lebanon imepongeza maandamano ya kijasiri ya "watu milioni moja" ya Wairani mnamo Januari 12, ambayo yalizima njama za maadui za kuivuruga nchi hii.
Katika sehemu ya mwisho ya taarifa yao wawakilishi wanaounga mkono Muqawama wametoa wito kwa serikali ya Lebanon kukabiliana na uchokozi wa utawala wa Kizayuni wa Israel na kuanza kwa dhati mchakato wa kujenga upya maeneo yaliyoathirika kama kipaumbele cha kitaifa, huku wakisisitiza umuhimu wa kuliepusha suala hilo na migogoro ya kisiasa.
3496152