IQNA

Vikosi vya Hashd al-Shaabi vya Iraq vaanza utekelezaji wa mpango maalum wa huduma kwa ajili ya Arbaeen

16:33 - July 18, 2026
Habari ID: 3482501
IQNA – Vikosi vya Hashd al-Shaabi (Jeshi la Kujitolea la Wananchi) vya Iraq vimetangaza siku ya Ijumaa kuwa vimeanza kutekeleza mpango maalum wa kuhudumia mamilioni ya mazuwaru wanaoelekea kwenye matembezi ya Arbaeen.

Utekelezaji wa mpango huu umeanza kabla ya kuanza rasmi kwa safari ya kila mwaka ya Arbaeen, kufuatia maagizo ya Abdulaziz Al-Mohammadawy, Mkuu wa Wafanyakazi wa Hashd al-Shaabi, na kwa uratibu wa karibu na Gavana wa Karbala, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na vikosi hivyo na kuripotiwa na Shirika Rasmi la Habari la Iraq (INA).

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mashine maalum na askari wametumwa kwenye maeneo ya misheni katika sehemu mbalimbali za mji mtukufu wa Karbala ili kufanya shughuli za usafi, kutengeneza barabara, kusaidia taasisi za huduma, na kuandaa mazingira bora ya kuwahudumia mamilioni ya mazuwaru wa Arbaeen.

Taarifa hiyo iliongeza: “Hatua hizi zinafanyika ndani ya mfumo wa mpango mpana wa huduma na kwa uratibu na taasisi za serikali, usalama, na huduma. Lengo letu ni kutoa huduma bora zaidi, kuunga mkono juhudi za utawala wa mkoa, na kuhakikisha kuwa ziara tukufu ya Arbaeen inafanikiwa kwa namna bora zaidi.”

Arbaeen ni tukio adhimu la kidini linaloadhimishwa na Waislamu wa madhehebu ya Shia katika siku ya arubaini baada ya Siku ya Ashura, kukumbuka kilele cha majonzi na kuuawa shahidi Imam Hussein (AS), mjukuu wa Mtume Muhammad (SAW) na Imamu wa tatu wa Mashia.

Hii ni moja ya ziara kubwa zaidi za kila mwaka duniani, ambapo mamilioni ya Waislamu wa Shia, pamoja na baadhi ya Waislamu wa Kisuni na wafuasi wa dini nyingine, husafiri kwa miguu kuelekea Karbala wakitokea miji mbalimbali ya Iraq na nchi jirani. Mwaka huu, siku ya Arbaeen itaadhimishwa tarehe 4 Agosti.

3498309/

captcha