IQNA

Hamas yaonya kuhusu njama mpya za Marekani dhidi ya Quds Tukufu

18:31 - December 23, 2017
Habari ID: 3471321
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas, Ismail Haniya ametoa indhari kuhusu njama mpya za Marekani dhidi ya mji wa Quds (Jerusalem).

Akizungumza Jumamosi mjini Ghaza, Kiongozi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas, Ismail Haniya amesema, mji wa Quds (Jerusalem) ulioungana ni mji mkuu wa nchi huru ya Palestina na nchi za Kiislamu na Kiarabu hazitaipuuza Quds.

Haniya ameyasema hayo leo katika Mkutano wa 11 wa Kimataifa wa Quds katika mji wa Ghaza. Ameongeza kuwa, kile ambacho kinajiri leo Palestina si Intifadha au mwamko tu bali ni Intifadha ya dunia nzima dhidi ya adui. Amesema ni kwa msingi huo ndio aghalabu ya nchi za dunia zikabainisha mtazamo wao katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na kupinga hatua ya Marekani kutambua Quds kama mji mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel.

Haniya ambaye ni Mkuu wa Idara ya Kisiasa ya Hamas ameendelea kusema kuwa Quds ni nembo ya kidini ya Palestina na kwa msingi huo kuna vita vigumu baina ya Wapalestina na utawala wa Kizayuni wa Israel katika kuulinda mji huo. Amesema Wazayuni wanatekeleza njama za kuibua nembo bandia za kidini na kihistoria katika Quds Tukufu ili hatimaye kunyakua kikamilifu mji huo.

Kiongozi huyo wa Hamas amesisitiza kuwa, Quds ni mji mkuu wa kisiasa wa taifa la Palestina na pia ni mji mkuu wa kidini wa Waislamu wote duniani. Halikadhalika amesema Quds ni mji mkuu wa wanadamu, maadili, thamani za wote watakao uhuru wawe ni Waislamu au Wakristo. Halikadhalika amesema Wapalestina hawatafanya mazungumzo kuhusu hatima ya Quds.

Ismail Haniya amesema leo watu wa Palestina wanapaswa kuchukua maamuzi imara ya kuvunja njama za Marekani. Kiongozi wa Hamas pia ametahadahrisha kuhusu njama ya Marekani ya kuitambua Israel kama dola la Kiyahudi na kuwanyima ruhusu ya kurejea makwao mamilioniya Wakimbizi Wapalestina walio katika nchi mbali mbali duniani.

Disemba sita Rais Donald Trump wa Marekani alitangaza kuwa eti Quds ni mji mkuu wa utawala haramu wa Israel hatua ambayo imepingwa n aghalabuya nchi duniani.

Baada ya Trump mwenyewe kutoa vitisho dhidi ya dunia nzima, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Alhamisi liliulaani kwa wingi mkubwa wa kura uamuzi wa rais huyo wa Marekani wa kuitangaza Baitul Muqaddas kuwa mji mkuu wa Israel. Katika upigaji kura wa kihistoria, nchi 128 wanachama wa Umoja wa Mataifa walilipigia kura za 'ndiyo' azimio hilo la Quds, wanachama tisa, walioipiga kura za 'la' na nchi nyengine 31 ziliamua kutopiga kura huku nchi zingine 21 zikikosa kushiriki katika kikao.

Uamuzi huo wa Baraza Kuu la Umoja wa Matiafa umefasiriwa kuwa ni fedheha kwa Marekani na ishara ya kuzidi kutengwa utawala wa nchi hiyo unaoognozwa na Trump.

3675336

captcha