Katika taarifa, Kamati ya "Al Quds na Mazungumzo" katika Kituo cha Kiislamu cha Al Azhar imesema kadhia ya ukombozi wa ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Israel itaendelea kuwa suala muhimu zaidi kwa Waislamu na Waarabu.
Kamati hiyo imelaani vikali hatua ya walowezi Waisraeli kuvamia Msikiti wa Al Aqsa chini ya ulinzi wa askari wa utawala wa Kizayuni wa Israel.
Aidha Al Azhar imelaani matembezi ya kichochezi ya walowezi Waisraeli katika mitaa ya Al Khalil (Hebron) hasa karibu na Msikiti wa Nabii Ibrahim AS siku ya Jumatatu.
Kamati hiyo imesema Waarabu na Waislamu duniani kote hawatasahau namna ardhi zao zinavyokaliwa kwa mabavu na Wazayuni na kwamba kadhia ya kupigiania ukombozi wa Palestina itaendele akuwa kadhia nambari moja.
Kamati hiyo imesema sera za utawala wa Kizayuni za kujaribu kubadilisha muundo asili wa Kiarabu na Kiislamu wa Quds hazitafauli.
Kamati ya "Al Quds na Mazungumzo" katika Kituo cha Kiislamu cha Al Azhar pia imetoa wito kwa viongozi wa dunia walaani ugaidi na ubaguzi wa Israel dhidi ya watu wasio na ulinzi wa Palestina.