IQNA

Mwanazuoni:Maombolezo ya Imam Hussein (AS) yanaendelea kuihuisha Uislamu

17:04 - June 17, 2026
Habari ID: 3482370
Mwanazuoni:Maombolezo ya Imam Hussein (AS) yanaendelea kuihuisha Uislamu
IQNA – Maombolezo ya Muharram si vitendo vya huzuni tu; bali kwa Waislamu wa madhehebu ya Shia kote duniani, ni uhai wa imani iliyodumu kwa karne kumi na nne, amesema mwanazuoni mmoja wa Kiislamu.

Hujjatul-Islam Mohammad Masjed-Jamei, mwanazuoni wa dini na mhadhiri katika Chuo cha Mahusiano ya Kimataifa cha Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, alisema katika mahojiano kuwa maombolezo ya kidini yamekuwa na nafasi kubwa katika kudumisha utambulisho wa Kishia.

Kisa hiki kinaanzia katika jangwa la Karbala, mwaka 61 Hijria (680 Miladia). Imam Hussein (AS), mjukuu wa Mtume Muhammad (SAW), alikataa kula kiapo cha utiifu kwa mtawala dhalimu Yazid ibn Muawiyah. Siku ya kumi ya Muharram, Ashura, Imam Hussein (AS), familia yake, na kundi dogo la masahaba na wafuasi wake watiifu walizingirwa na kuuawa kikatili na jeshi kubwa lililowazidi mno kwa idadi na nguvu. Kuuawa kwake shahidi hakukuwa mwisho wa harakati; bali ilikuwa mwanzo wake.

Hujjatul-Islam Masjed-Jamei amebainisha kuwa kuendelea kuwepo kwa Uislamu wa Kishia hakutenganishwi na juhudi za Maimamu waliokuja baada yake katika kulihifadhi kwa vitendo kumbukumbu ya Ashura.

“Kilichoifanya Ashura iendelee kuwa hai na kuupa Uislamu wa Kishia uhai wake wa kipekee ni kwamba Maimamu, baada ya Ashura, walifanya juhudi za kuihuisha kupitia maombolezo, kwa kusimulia fadhila na utukufu wa Imam Hussein, na kwa kuadhimisha siku hii,” alisema. “Harakati hii ilikuwa na taathira kubwa mno. Kuendelea kwa Uislamu wa Kishia kwa kiasi kikubwa kunatokana na maombolezo ya Imam Hussein.”

Alitoa mfano wa zama za Imam Ja’far al-Sadiq (AS), Imam wa sita wa Kishia. Mshairi mmoja alimjia Imam, naye akamuelekeza asome beti kuhusu msiba wa Imam Hussein, huku pazia likiwekwa baina ya wanaume na wanawake. Masjed-Jamei alibainisha: “Alimwambia: soma kwa lahaja yenu ya kienyeji.”

Alieleza kuwa wakati huo, maombolezo yalikuwa bado hayajawa mfumo rasmi wa kijamii na kidini. Lakini kizazi baada ya kizazi, yalipanuka na kuwa muundo mkubwa wa kitamaduni.

Muundo huo, Masjed-Jamei aliendelea kusema, sasa umeenea katika mabara na karne mbalimbali , kuanzia hotuba na majlisi za mawaidha, hadi mikusanyiko ya majumbani, maadhimisho ya misimu maalumu, na matembezi ya Arbaeen, mojawapo ya mikusanyiko mikubwa zaidi ya kila mwaka ya wanadamu duniani, inayofanyika siku 40 baada ya Ashura.

Katika nchi kama India, Pakistan, Afghanistan, na Iran, ibada na maadhimisho haya yamekuwa “utamaduni, taasisi, ada, na sehemu ya dini yenyewe.”

Nchini Iran, ambako Uislamu wa Kishia ndio dini rasmi ya taifa, namna ya kuueleza utamaduni huu imekita mizizi kwa kina zaidi. Sanaa za kale kama Ta’zieh, maigizo ya kidini yanayosimulia tena tukio la Karbala , pamoja na desturi nyingine za maombolezo, zote zimechipuka kutoka katika mizizi ya huzuni ya Ashura.

“Iwapo mtu atashiriki kwa ikhlasi katika majlisi hizi, atapata utulivu wa kina wa kiroho,” alisema. “Tajiriba hii imehisiwa na matabaka yote , watu wa mijini na vijijini, vijana na wazee, wanaume na wanawake , na kupitia tajiriba hii wameweza kuutambua ukweli wa Uislamu wa Kishia.”

Alisisitiza kuwa huu ni urithi hai , uliokita mizizi katika damu ya Karbala, uliolishwa na kunyunyiziwa kwa karne nyingi za mapenzi na kujitolea, na ambao bado unaendelea kukua.

3497865

Kishikizo: imam hussein as ashura
captcha