IQNA

Wasichana wadogo washiriki Mashindano ya Qur'ani Tukufu huko Najaf

15:16 - February 27, 2026
Habari ID: 3482003
IQNA – Kituo cha Dar‑ul‑Qur'an cha Wanawake, kinachohusiana na Idara ya Usimamizi wa Haram Tukufu ya Imam Ali (AS), kinaandaa mashindano ya Qur'ani Tukufu kwa wasichana wadogo katika mji mtukufu wa Najaf.

Mashindano hayo, yaliyopewa jina la “Kiumbe Bora Zaidi”, yanafanyika katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na yanajumuisha hifdhi (uhifadhi) na tafsiri ya Surat Al‑Bayyinah.

Mashindano haya yamelenga wasichana wenye umri wa miaka 6 hadi 13, na yameandaliwa kwa mfumo usio wa ana kwa ana, yakilenga kuimarisha uwezo wa Qur'ani wa kizazi kipya kwa njia inayolingana na umri wao.

Waandaaji wamesisitiza kuwa mashindano hayo yamepangwa kwa mtazamo wa kielimu unaozingatia hatua za ukuaji wa watoto, ili kuwasaidia kuelewa Qur'ani Tukufu kwa upole, hekima na mapenzi.

Programu hii na nyingine kama hizi zinalenga kuongeza ufahamu wa watoto kuhusu mafundisho ya Qurani, kuimarisha ujuzi wao wa kusoma na kuhifadhi Qur'ani, na kuimarisha uhusiano wao wa kiroho na Neno la Wahyi tangu wakiwa wadogo.

Bi Dalal Al‑Tabatabai, mkuu wa Kituo cha Dar‑ul‑Quran cha Wanawake, alisema kuwa mashindano yanafanyika kwa njia ya mtandao kupitia programu ya Telegram, na mada zake ni pamoja na kuhifadhi aya, kufasiri maneno ya Qur'ani, na kufundisha kanuni za usomaji sahihi (tajwid).

Kwa mujibu wa Al‑Tabatabai, hatua ya mwisho ya mashindano itafanyika tarehe 15 ya Ramadhani, sambamba na maadhimisho ya kuzaliwa kwa Imam Hassan Mujtaba (AS).

Akisisitiza umuhimu wa utekelezaji wa programu kama hizi, alizitaja kuwa ni aina ya uwekezaji wa Qur'ani katika utoto, unaounganisha elimu na malezi ya vipaji, na kuweka msingi wa kutambua na kulea vipawa vya baadaye vya Qur'ani.

Aliongeza kuwa shughuli hizi zinafanyika kwa kuzingatia dhamira ya Kituo cha Dar‑ul‑Quran cha Wanawake ya kulea kizazi cha Qur'ani, na kuimarisha maadili ya imani katika nyoyo na maisha ya watoto tangu umri mdogo.

Mashindano haya ni sehemu ya mfululizo wa matukio ya Ramadhani yanayoandaliwa kila mwaka na kituo hicho, kwa lengo la kuunga mkono elimu ya Qur'ani Tukufu na kuimarisha ushiriki makusudi wa wasichana katika shughuli na matukio maalumu ya Qur'ani.

3496578

Habari zinazohusiana
captcha