IQNA

Matukio ya Palestina

HAMAS yakamata ndege ya kijasusi ya utawala haramu wa Israel

19:12 - January 31, 2023
Habari ID: 3476496
TEHRAN (IQNA)- Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) imefanikiwa kutwaa ndege isiyo na rubani ya kijasusi ya utawala haramu wa Israel iliyokuwa ikiruka katika anga ya Ukanda wa Gaza.

Brigedi ya Izzudeen Qassam, tawi la kijeshi la HAMAS imesema katika taarifa kuwa, wahandisi wa harakati hiyo ya muqawama ya Palestina wamefanikuwa kupata taarifa 'hasasi' na muhimu kutoka kwenye droni hiyo aina ya hexacopter ya Wazayuni.

Utawala pandikizi wa Israel umekuwa ukikwepa kulizungumzia suala hili la kutwaliwa droni yake ya kijasusi na wanamuqawama wa Palestina. HAMAS imebainisha kuwa, droni hiyo ya kijasusi ilitwaliwa na Bridegi ya Qassam alfajiri ya Ijumaa iliyopita ikiruka katika anga ya Ukanda wa Gaza. 

Baada ya HAMAS kufichua habari ya kutwaliwa droni hiyo, utawala haramu wa Israel kupitia msemaji wake hatimaye ulikiri kuwa, 'kitu kinachofanana na droni yake' kimetua Gaza. 

Katika miezi ya hivi karibuni, ndege zisizo na rubani, ndege za kijeshi, helikopta na mizinga ya utawala wa Kizayuni imekuwa ikitumika kufanya mashambulizi katika maeneo mbalimbali ya Ukanda wa Gaza. HAMAS imefanikiwa kutungua akthari ya droni hizo za Wazayuni.

Makundi ya muqawama ya Palestina yanasisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni unatumia kila nyenzo ya ukatili na utumiaji mabavu kulipgisha magoti taifa la Palestina, lakini Wapalestina hawatasalimu amri katu, na wako tayari kukabiliana na Wazayuni wakati wowote na mahali popote.

Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS inasisitiza kuwa, jinai za kila uchao za utawala huo wa Kizayuni hazitapita hivi hivi bila kupatiwa majibu.

Israel yakaribia kupromoka

Mtafiti wa Kizayuni Profesa Daniel Kahneman amekosoa hatua za baraza la mawaziri la mrengo wa kulia wenye misimamo ya kufurutu mpaka linaloongozwa na waziri mkuu wa utawala haramu wa Israel Benjamin Netanyahu hususan kuhusiana na mageuzi ya Idara ya mahakama na kusema kuwa, hatua hizo zinamaanisha kumomonyoka ndani kwa ndani na kumalizika utawala wa Kizayuni.

Maelfu ya Wazayuni katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina zilizopewa jina la Israel, wamekuwa wakiandamana kwa wiki kadhaa sasa, huku kila Jumamosi usiku wakifanya hivyo huko Tel Aviv na katika miji mingine kadhaa ya ardhi zinazokaliwa kwa mabavu wakipinga kile walichokiita "mapinduzi ya kisiasa" na kulalamikia maamuzi na sera za baraza la mawaziri lenye misimamo ya kufurutu ada linaloongozwa na Netanyahu

Vyombo vya habari vya Kizayuni vimekadiria idadi ya waandamanaji kuwa makumi ya maelfu.

Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA, Profesa Daniel Kahneman, mtafiti wa Kizayuni aliyeshinda Tuzo ya Nobeli ya Uchumi mwaka 2002, ameeleza katika mahojiano na chaneli ya 12 ya utawala wa Kizayuni kwamba, hivi sasa ana wasiwasi zaidi na hali ya utawala huo kuliko alivyokuwa wakati wa vita vya Oktoba 1973. 

Akiashiria mpango wa baraza la mawaziri lenye misimamo ya kufurutu mpaka la Netanyahu wa kutekeleza mageuzi katika mfumo wa mahakama, ambayo yamesababisha maandamano makubwa ya upinzani katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu, Kahneman amesema, "kinachonitia wasiwasi zaidi ni mapinduzi ya idara ya mahakama".

Mtafiti huyo wa Kizayuni ameongezea kwa kusema, "kwa maoni yangu, huu ni mwisho wa dunia na mwisho wa Israel niliyokuwa nikiijua mimi". Kahneman amefafanua kwa kusema, "nikilinganisha kiwango cha wasiwasi wangu juu ya Israel nimebaini kuwa, wasiwasi nilionao sasa ni mkubwa zaidi kuliko wakati wa vita vya Oktoba 1973 (vita kati ya Waarabu na utawala wa Kizayuni). Wakati ule sikuwa na wasiwasi kiasi hiki, ilhali sasa hivi nina wasiwasi juu ya dhati ya Israel yenyewe".

Jumla ya Wapalestina 35 wameuliwa shahidi na Israel mwezi Januari pekee

Wizara ya Afya ya Palestina imetangaza kuwa, mwezi Januari mwaka huu ndio mwezi uliojaa umwagaji damu mkubwa zaidi katika eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan baada ya utawala wa Kizayuni wa Israel kuwaua shahidi Wapalestina 38.

Wazayuni kila siku hushambulia maeneo mbalimbali ya Palestina ili kufanikisha malengo yao ya kujitanua; ambapo hadi sasa Wapalestina wengi wameuawa shahidi au kujeruhiwa na wanajeshi wa utawala haramu wa Israel.  

Wizara ya Afya ya Palestina imetangaza kuwa, mwezi uliopita wa Januari ndio mwezi ulishuhudia umwagadi mkubwa wa damu katika eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan tangu mwaka 2015 hadi sasa, kufuatia kuuliwa shahidi Wapalestina 35 wakiwemo watoto 8. Raia hao wa Palestina wameuawa kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa utawala ghasibu wa Israel na walowezi wa Kiyahudi. 

Wizara ya Afya ya Palestina imeongeza kuwa, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni waliwalenga na kuwashambulia Wapalestina wengi katika eneo hilo. Imeongeza kuwa, tangu kuanza mwaka huu wa 2023, Wapalestina 20 wameuliwa shahidi katika mji wa Jenin. Idadi hiyo ni kubwa kuwahi kusajiliwa huko Jenin. 

Ni zaidi ya miaka 70 sasa utawala ghasibu wa Israel unaendelea kutwaa na kughusubu haki za wananchi madhlumu wa Palestina. Katika miaka yote hiyo utawala haramu wa Israel umetenda jinai nyingi za kutisha na za kinyama dhidi ya Wapalestina. 

Jihadul-Islami: Wapalestina hawakhofu walowezi wa Kizayuni kuzatitiwa kwa silaha

Mjumbe wa ofisi ya kisiasa ya harakati ya Jihadul-Islami ya Palestina amesema kuwa, Wapalestina hawaogopi wala hawaingiwi na hofu yoyote kwa sababu ya walowezi wa Kizayuni kuzatitiwa kwa silaha.

Chaneli ya 14 ya televisheni ya utawala wa Kizayuni wa Israel imekiri kuwa, kuanzia Jumamosi hadi sasa makundi ya muqawama ya Palestina yamefanya operesheni 57 dhidi ya Wazayuni katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Baitul Muqaddas inayokaliwa kwa mabavu.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Falastin Al-Youm, Muhammad al-Hindi, mjumbe wa ofisi ya kisiasa na mkuu wa kitengo cha siasa cha harakati ya Jihadul-Islamu amesema, taifa la Palestina halitasalimu amri kwa hujuma na uchokozi wa utawala wa Kizayuni na lina azma thabiti ya kukabiliana nao katika miji yote ya Palestina.

Al-Hindi amesema, anatazamia Israel itachukua hatua kutokana na operesheni ya kishujaa ya Quds na akaongeza kuwa, taifa la Palestina liko tayari kwa lolote linalowezekana kutokea.

Mjumbe huyo wa Jihadul-Islami amesisitiza kuwa, uamuzi wa Wazayuni wa kuwapa silaha walowezi wa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Baitul Muqaddas hauwatii hofu wala woga Wapalestina, na maamuzi ya hivi karibuni ya Benjamin Netanyahu, waziri mkuu wa baraza la mawaziri lenye misimamo ya kufurutu mpaka la utawala huo ghasibu yanachukuliwa kwa lengo la kuwapoza na kuwatuliza wazayuni.

Al-Hindi ameongeza kuwa, taifa la Palestina halitasalimu amri kwa hujuma na uvamizi wa Israel, na kwamba operesheni ya Ijumaa usiku huko Quds iliyopelekea kuangamizwa Wazayuni wasiopungua wanane, ilikuwa jibu kwa uchokozi na jinai za mtawalia za Wazayuni.

Al-Hindi amesema, utawala ghasibu wa Kizayuni unatumia kila nyenzo ya ukatili na utumiaji mabavu kulipgisha magoti taifa la Palestina, lakini Wapalestina hawatasalimu amri katu. Ameongeza kuwa, taifa la Palestina halitasalimu amri kwa adui Mzayuni na liko tayari kukabiliana naye wakati wowote na mahali popote.

Jumamosi usiku, wakazi wa Ukanda wa Gaza walionyesha furaha yao kwa operesheni ya kishujaa iliyotekelezwa Quds kwa kugawa vitafunio vitamu na kupiga nara za Takbir huku wakiwa wamebeba bendera za Palestina.

4118359

Habari zinazohusiana
Kishikizo: jinai za israel
captcha