IQNA

Zaidi ya Waislamu Milioni 18.5 walitekeleza Ibada za Hija na Umrah nchini Saudia mwaka jana

18:41 - April 25, 2025
Habari ID: 3480591
IQNA – Saudi Arabia imetangaza kuwa zaidi ya Waislamu milioni 18.5 walitekeleza ibada za Hija na Umrah mwaka uliopita.

Tawfik Al Rabiah, Waziri wa Hija na Umrah, alitoa tangazo hili wakati wa hotuba katika Kituo cha Oxford cha Masomo ya Kiislamu nchini Uingereza. Alisisitiza kuhusu hatua kadhaa za kuboresha huduma kwa Mahujaji, ikiwa ni pamoja na majukwaa ya kidijitali yaliyoundwa ili kurahisisha safari zao. 

Miongoni mwa hatua hizi ni mfumo wa elektroniki wa ufuatiliaji, uliotengenezwa kwa ushirikiano na zaidi ya nchi 80, na jukwaa la Nusuk, linalofanya kazi katika mataifa 126. Hili la mwisho linawawezesha wanaokusudia kutekeleza Hija na Umrah kupanga safari zao bila kutegemea huduma za madalali. Jukwaa hili pia husaidia na mipango ya kimsingi kama vile kupata makazi kwa wale wanaotembelea Makka kwa Umrah au mji wa Madina, ambao una eneo la pili takatifu zaidi kwa Uislamu. 

Hatua nyingine iliyotangazwa ni matumizi ya kadi za kielektroniki zinazojumuisha taarifa za binafsi na afya za Mahujaji, kwa lengo la kurahisisha usafiri wao na kuongeza usalama. 

Al Rabiah pia alitaja matumizi ya Akili Mnemba (AI) ndani ya Msikiti Mkuu wa Makka—mahali pa ibada patakatifu zaidi kwa Uislamu—ili kufuatilia mienendo ya umati na kushughulikia dharura kwa ufanisi huku ikihifadhi utakatifu wa eneo hilo. 

Apu ya Nusuk, inayotoa zaidi ya huduma za kidijitali 100 katika lugha 20, inasemekana kuwa imetoa vibali zaidi ya milioni 13 vya kutembelea Al Rawda Al Sharifa huko Madina,mahali ambapo kaburi la Mtume Muhammad (SAW) lipo, ikilinganishwa na milioni 4 mnamo 2022. Mahujaji wengi wanaosafiri kwa Umrah katika Msikiti Mkuu wa Makka yaani Masjid al Haram baadaye husafiri hadi Madina kusali katika Msikiti wa Mtume, Al Masjid An Nabawi. 

Wakati Saudia inajiandaa kwa msimu ujao wa Hija , Wizara ya Hija imeweka tarehe 29 Aprili—siku ya kwanza ya mwezi wa Kiislamu wa Dhul Qadah—kama tarehe ya mwisho kwa Mahujaji wa kimataifa wa Hija ndogo ya Umrah wa kuondoka nchini humo. 

Ibada ya kila mwaka ya Hijja ya mwaka 2025 inatarajiwa kufanyika mapema Juni, na tarehe kamili zitategemea kuonekana kwa mwezi kwa mwezi wa Kiislamu wa Dhul Hijjah. Mamlaka za Saudia kawaida huthibitisha ratiba ya Hijja karibu na tukio, kwa kuwa miezi ya kalenda ya Kiislamu ya mwandamo ni takriban siku 10-12 fupi kuliko kalenda ya Kigrigori, na hivyo kusababisha ibada za Hijja kuhama mapema kila mwaka. Mwaka 2024, Hijja ilifanyika katikati ya Juni, na ibada za mwaka ujao zinatarajiwa kuanza karibu na tarehe 6 Juni, 2025, zikidumu siku tano.

3492828

Habari zinazohusiana
captcha