Seyed Hassan Hosseini amesema kuwa anatarajia mahudhurio ya watu milioni 15 katika maandamano hayo ya mazishi.
Akizungumza katika kikao cha Baraza la Utawala la Mji wa Mashhad siku ya Jumatatu, alisema kuwa nchi nzima imejitayarisha kwa ajili ya tukio hili kubwa na la kihistoria la kumuaga Kiongozi huyo aliyekufa shahidi.
Alibainisha kuwa mji wa Mashhad umekuwa kitovu cha matukio mengi muhimu ya kihistoria, kisiasa, na kiutamaduni nchini Iran, na tukio hili litakuwa ni mgeuko muhimu katika historia ya mji huo.
“Sote tunapaswa kushirikiana ili shughuli hii ifanyike kwa namna bora zaidi. Kwa bahati njema, mji wa Mashhad una uwezo mkubwa wa kupokea watu, na ni wajibu wetu kuwakaribisha vyema mazuwari na wageni watakaohudhuria shughuli hii. Wageni hawa ni baraka kubwa kwa mji wa Mashhad, na kwa sasa asilimia 80 ya uwezo wa hoteli zetu tayari umeshajaa.”
Hosseini aliongeza, “Tutaisafisha na kuiandaa njia ya mazishi ipasavyo, na tunatabiri kuwa watu milioni 15 watahudhuria mazishi hayo. Ofisi ya Gavana inaunga mkono kikamilifu shughuli hii, na tumejiandaa na mahitaji yote muhimu kwa ajili ya kuwapokea wananchi.”
Alifafanua zaidi kuhusu malazi ya mazuwari, akisema kuwa mji huo umeandaa sehemu za malazi kwa ajili ya watu milioni 1.5, na “tuko tayari kuongeza uwezo huo. Tunatabiri kuwa mazuwari na wageni wa shughuli hii ya mazishi watakuwepo jijini kwa muda wa hadi wiki nzima. Hatujawahi kushuhudia uwepo wa idadi kubwa kama hii ya watu katika mji wa Mashhad hapo awali, hivyo tusishangae na tuwe tayari kuwahudumia kwa heshima.”
4359860